RABAT, Morocco
KIUNGO wa kati wa Morocco, Azzedine Ounahi ametajwa kuwa miongoni mwa nyota wanaotarajiwa kutazamwa zaidi katika Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025.
Michuano hiyo imepangwa kuanza kufanyika Desemba 21, mwaka huu nchini Morocco.
Morocco imepangwa kundi A na timu za Mali, Zambia na Comoros katika michuano hiyo yenye kuvuta hisia kubwa kwa mashabiki wa soka Barani Afrika na hapa nchini.
Morocco maarufu ‘Atlas Lions’ katika michuano hiyo hii, inasaka taji hilo kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1976.
Tayari Ounahi ameibuka kama mtu muhimu katika kampeni za wenyeji kuhakikisha safari hii taji hilo linabakia nchini Morocco.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25, jukumu lake limekuwa na uzito zaidi huku kukiwa na sintofahamu juu ya utimamu wa nahodha Achraf Hakimi.
Kama Hakimi atakosa kushiriki michuano hiyo, Ounahi atakuwa na jukumu la kuongoza maeneo ya kati kuhakikisha Morocco inafanya vizuri katika mashindano hayo.
Hatua hiyo, inakuja baada ya Ounahi kupita kipindi kigumu huko Marseille, lakini hivi sasa Ounahi amejiimarisha tena kama mwanzilishi wa kawaida tangu ajiunge na timu ya Girona.
Baadhi ya mashabiki wa soka nchini Morocco wanamwona mchezaji huyo kama nyota anayeweza kuunda bahati ya timu katika ardhi ya nyumbani kutwaa taji hilo.
Wachezaji wengine wanaotarajiwa kung’ara katika michuano hiyo ni Mohamed Salah wa Misri.
Victor Osimhen wa Nigeria, Riyad Mahrez wa Algeria na Sadio Mané wa nchi ya Senegal.
Pia, imeelezwa kuwa katika fainali hizo wapo chipukizi wa kuangaliwa ambao ni Ibrahim Mbaye wa Senegal na Rogers Mato wa Uganda.




