Na NASRA KITANA
MWENYEKITI wa Bodi ya Wakurugenzi wa Klabu ya Simba, Clesentius Magori amesema pamoja ya ugumu na changamoto walizopitia, hatimaye mchakato wao wa mabadiliko ya klabu hiyo unakaribia kukamilika.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Magori amesema wanafurahi kuona mchakato huo unaenda kufikia tamati baada ya kupitia changamoto kwa miaka minane.
Amesema mabadiliko hayo, yamekuwa na ugumu na misukosuko mingi tangu mwaka 2017, lakini ni muhimu kwa maendeleo ya klabu katika kuhakikisha Simba inadumisha mafanikio yake ndani na nje ya nchi.
“Napenda kuwaambia kwamba mchakato wa mabadiliko ulioanza 2017, hivi sasa unakwenda kufikia tamati, ni kipindi kigumu tumepita, ukiacha Ujerumani hakuna sehemu nyingine unatumika, hivyo tumeona changamoto ilivyokuwa namna ya kuupitisha, unaitwa ‘Hybrid’.
“Kulikuwa na changamoto mbalimbali mpaka mchakato kufikia hapa, lakini tumepita sehemu tofauti tofauti na hatimaye mwanasheria mkuu wa serikali amesisitiza tukae na Baraza la Michezo la Taifa (BMT) tuyamalize, hili ni kubwa kwa Simba na hivi sasa ndiyo tunaanza safari ya kumaliza mchakato huo,” amesema Magori.
Amefafanua kuwa kikao chao cha mwisho kilipitisha katiba ambayo kuanzia kesho wanaanza kutengeneza katiba mpya, ni jambo kubwa Simba, kwani wamepitia kipindi cha miaka minane ya kupanda na kushuka.
“Sasa wataingia makubaliano ya kujua mwekezaji atafanya nini na wanachama watafanya nini,”alisema.
Hata hivyo, Magori alisema baada ya kukaa miaka minane bila kufanya usajili wa wanachama wapya, Simba imetangaza kufufua mchakato huo hivi karibuni kwa kusajili idadi kubwa zaidi Tanzania.
“Kubwa ambalo wanakwenda kulifanya tulikuwa tumesimamisha usajili wa wanachama lakini hivi sasa tunakwenda kutoa kadi za wanachama, hivyo tutakuwa klabu ya kwanza yenye wanachama wengi, siyo tu Tanzania,” alisema Magori.
Katika hatua nyingine, Magori alisema kuwa uongozi wa Simba uko imara na hakuna migogoro baina yao kama ambavyo imekuwa ikiripotiwa.
Vuguvugu la mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji wa Simba lilianza Julai 2016, wakati Rais wa Heshima wa Klabu hiyo
Mohamed Dewji ‘Mo’ alipotangaza nia ya kutaka kuwekeza kwa kiwango cha hisa cha asilimia 50 alizotangaza atazinunua kwa kiasi cha sh. bilioni 20.
Suala hilo la Dewji liliibua vuguvugu ndani ya klabu hiyo ambapo lilikuja kusababisha kubadilishwa kwa katiba yake na kupatikana mpya ambayo inabariki mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji, Simba iwe kampuni huku mfanyabiashara huyo akishinda zabuni ya kuwa mwekezaji kwa asilimia 49 ya hisa za klabu hiyo.
TIMU KUTOFANYA VIZURI
Magori alisema kuwa chanzo kikubwa cha timu kushindwa kufanya vizuri ni kutokana na changamoto ya mabadiliko ya kocha na baadhi ya wachezaji kuwa majeruhi.
“Kiufundi, timu iliyumba kwa sababu kocha aliyekuwa amezindua msimu aliondoka kwani hakukidhi vigezo,” alisema Magori.
KOCHA MPYA
Katika hatua nyingine, Simba imemtangza raia wa Afrika Kusini, Steve Becker kuwa kocha mpya wa timu akirithi mikoba ya Dimatar Pantev
Kocha huyo ametia saini mkataba wa mwaka mmoja, ambapo kabla ya kutua Msimbazi, alishawahi kupita katika timu za University of Pretoria 2008–2014, AmaZulu 2014–2016 na Stellenbosch 2017–hadi mwaka huu.
Kocha huyo ana miaka 57, atajiunga na Simba mapema ili kujumuika na wachezaji katika mashindano ya Kombe la Mapinduzi.
Michuano hiyo imepangwa kuanza Desemba 28, mwaka huu hadi Januari 13, mwakani huko visiwani Zanzibar.




