Na IGAMBA LIBONGE, Kilombero
KAYA 150 zimeathirika kutokana na mafuriko, kufuatia mvua kubwa zinazoendelea kunyesha Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro.
Maeneo yaliyoathirika zaidi ni Mabukula (Kata ya Kibaoni), Kata za Lumemo, Michenga, Mbasa, Kiberege, Mbingu na Chita.
Akizungumza na UHURU, Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Dunstan Kyobya, amesema vikosi vya uokoaji vipo eneo la tukio kusaidia wananchi walioathirika.
Kyobya amesema hadi sasa, hakuna taarifa ya vifo vilivyoripotiwa, baada ya kutembelea maeneo yaliyoathirika, ambapo alitoa rai kwa wananchi wanaoishi mabondeni kuhama kwa muda kwenda sehemu salama kuepuka madhara.
Aidha, Kyobya amewataka wananchi hao kuchukua tahadhari dhidi ya magonjwa ya mlipuko, yanayoweza kutokea kufuatia mvua hizo.
Katika Kata ya Mbingu mafuriko hayo yamesababisha athari kubwa baada ya kuharibu makazi, miundombinu ya barabara na mali za wananchi.
Pia, maji yamejaa maeneo mengi na kusababisha kukatika mawasiliano ya barabara, hatua iliyochangia ugumu wa upatikanaji huduma muhimu za kijamii.
Vilevile, Daraja la Rufuru linalounganisha Kata ya Chita na Mlimba, limevunjika usiku wa kuamkia jana na kukatisha mawasiliano ya barabara kati ya Ifakara na Mlimba.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba, Jamali Idrissa, alisema serikali inaendelea kuchukua hatua kwa kutoa msaada kwa waathirika wa mafuriko hayo.




