Na MWANDISHI MAALUMU
MAKAMU wa Rais, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, amesema suala la utekelezaji wa mabadiliko na uboreshaji uliofanyika katika sera ya elimu na mafunzo na mitaala, linahitaji ushirikiano wa hali ya juu miongoni mwa wadau wa elimu, taasisi za serikali na zisizo za serikali, wazazi na jamii.
Dk. Nchimbi alisema hayo jijini Dar es Salaam, alipofungua Kongamano la Kimataifa kuhusu uboreshaji wa sera ya elimu na mitaala nchini, linalofanyika ukumbi wa Maktaba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Aliitaka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kushirikiana na taasisi za elimu hususan Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuendelea kufanya ufuatiliaji na utafiti, kubaini dosari zozote zinazokwamisha utekelezaji wa suala hilo.
Pia, kubaini na kuibua maeneo yanayohitaji uboreshaji zaidi wa kiutendaji.
Makamu wa Rais alisema suala la utekelezaji wa mabadiliko na uboreshaji uliofanyika katika sera ya elimu na mafunzo na mitaala kuanzia elimu ya awali, msingi, sekondari hadi elimu ya juu.
Alisema utekelezaji huo unataka Watanzania kutafsiri vyema maono ya Dk. Samia Suluhu Hassan, kuhusu mfumo wa elimu unaozingatia kutoa ujuzi na maarifa, kumwezesha mhitimu kumudu mazingira yake na ushindani katika dunia ya kazi.
Dk. Nchimbi alisema suala la elimu jumuishi inayozingatia usawa ni miongoni mwa vipaumbele, ambapo serikali imeweka msisitizo katika uwepo wa vifaa vya kufundishia, kujifunzia na miundombinu rafiki kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu.
Alisema suala hilo linakwenda sanjari na uandaaji wa walimu wenye ujuzi wa elimu maalum kufundisha wanafunzi hao.
PROFESA ADOLF MKENDA
Waziri wa Elimu, Sayansi naTeknolojia, Profesa Adolf Mkenda, alisema kongamano hilo ni fursa nzuri ya ushirikishwaji wa watalaamu na wachambuzi kuangalia jinsi ambavyo utekelezaji huo unaendelea.
Alisema kongamano hilo litaangazia zaidi namna bora na ufanisi wa kutekeleza mageuzi ya elimu nchini.
PROFESA WILLIAM ANANGISYE
Akitoa taarifa kuhusu kongamano hilo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa William Anangisye, alisema malengo ya kongamano hilo ni kutafakari na kujenga uelewa wa pamoja miongoni mwa wadau kuhusu sera ya sasa ya elimu, mafunzo, marekebisho ya mitaala na athari zake kwa maendeleo endelevu.
Profesa Anangisye alisema lengo jingine ni kuibua mijadala ya kitaaluma kuhusu mitaala ya elimu ya msingi, sekondari na elimu ya juu, kutafakari kuhusu maendeleo ya kitaaluma na nafasi ya elimu ya ualimu kulingana na uboreshaji wa sera ya elimu na mafunzo, kubadilishana uzoefu wa kimataifa na kikanda jinsi uboreshaji wa elimu unavyochangia ukuaji jumuishi na mustakabali wa maendeleo endelevu.
Uboreshaji unaofanywa na serikali katika baadhi ya maeneo ya sera ya elimu na mafunzo, umefanyika kuondoa changamoto zilizokuwa zikiikabili elimu ya Tanzania, ikiwemo kujikita zaidi katika elimu ya nadharia, badala ya vitendo na kutokuwepo kwa fursa za elimu na mafunzo zinazozingatia mahitaji ya soko la ajira.
Vilevile, upungufu katika njia za ujifunzaji ambazo hazikukidhi hali halisi ya mazingira na maadili ya Kitanzania.





