Na ZIANA BAKARI
BAADHI ya wadau wakiwemo wasomi na wachumi, wamewashauri wananchi kuanza kuweka utaratibu wa kutunza akiba ya fedha kujiepusha na athari za kiuchumi pindi dharura zitakapojitokeza.
Pia, wametakiwa kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, badala yake, wajikite kuweka mipango mizuri ya maisha itakayowasaidia kukabiliana na changamoto za kiuchumi na kijamii.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na UHURU, baadhi ya wadau hao, waliwasihi wananchi kuweka akiba itakayosaidia kutatua changamoto zinapojitokeza.
DK. DANINGA
Mhandiri Mwandamizi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA), Dk. Philip Daninga, amesema hivi sasa ni kipindi cha sikukuu, ni vyema wananchi kukumbuka kuweka akiba.
Amesema kipindi cha sikukuu, matumizi yanakuwa mengi na kusababisha baadhi ya wananchi kusahau kuweka akiba ambayo ni jambo muhimu linalopaswa kupewa kipaumbele.
Akitaja madhara yanayoweza kutokea mtu asipoweka akiba, Dk. Daninga asema itasababisha migogoro ndani ya familia na mtu kushindwa kuendelea na shughuli zake za kila siku za kumpatia kipato.
Kwa mujibu wa Dk. Daninga, jamii inapaswa kujitahidi kuweka akiba kusaidia kuondokana na migogoro isiyo ya lazima ambayo haina umuhimu katika maisha.
“Migogoro ya familia inatokea pale suala la ada ya mtoto inapokuwa inahitajika na ukiangalia, hujaweka akiba inakuwa inasababisha mtafaruku ndani ya familia, muda mwingine inaweza kusababisha familia kuingia katika mikopo isiyo ya lazima ni vizuri tuweke akiba.
“Wazazi na walezi, tunapaswa kujua kuwa kuna leo na kesho je,? Tumejipanga vipi kwa sababu sherehe ni za muda mfupi, lakini maisha ni ya muda mrefu, yanapaswa kuwa na mipango endelevu,”alisema.
DK. TIMOTHY
Mhadhiri wa Uchumi kutoka Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Dk. Timothy Lyanga, aliishauri jamii kuweka utaratibu wa matumizi sahihi ya fedha, hususan kipindi hiki cha sikukuu na kufunga mwaka.
Alisema jamii inapaswa kutambua kuwa, umuhimu wa kutumia matumizi ya kawaida kwa kuwa, yanasaidia kuweka akiba itakayosaidia kutatua changamoto yoyote itakapojitokeza.
“Tujiepushe na matumizi yasiyo ya lazima, badala yake tujikite kuweka mipango mizuri ya maisha itakayotusaidia kukabiliana na tatizo lolote,”alisema.
DK. MAGUO
Mhandiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Dk. Mohamed Maguo, aliwashauri wananchi kuweka utaratibu wa kutunza akiba ambayo ni jambo muhimu.
Akizungumzia umuhimu wa kuweka akiba, Dk. Maguo alisema haiozi, bali inasaidia sehemu kubwa ya kukabiliana na changamoto yoyote itakapojitokeza.
“Niwaombe sana wananchi tusijisahau kuweka akiba, tunafahamu mwakani mwezi Januari, watoto watahitaji ada na wapo baadhi yetu, tunahitajika kulipa kodii, hii kwetu inapaswa iwe desturi kila mwananchi kuweka akiba,”alisema.
PROFESA WANGWE
Mtaalamu wa Uchumi, Profesa Samuel Wangwe, alisema kitu cha muhimu katika maisha ni namna nzuri ya kupangilia matumizi ya fedha.
Alisema kila mwananchi anapaswa kujua namna ya matumizi ya fedha yatakavyokuwa, siyo kuitumia bila malengo yoyote.
“Kila mmoja naamini ana malengo aliyojiwekea, hivyo ni vyema fedha tunazotumia zile katika malengo yale tuliyojiwekea na kukusudia tusitumie tu bila ya mpangilio wowote, hii haitaleta maendeleo,” alisema.
WASEMAVYO WANANCHI
Mkazi wa Vingunguti, Jijini Dar es Salaam, Rabia Hussein, aliwasihi wazazi wenzake, kuweka utaratibu wa kutunza akiba hususan kipindi hiki cha msimu wa sikukuu.
Alisema akiba ina umuhimu mkubwa kwa sababu, husaidia kutatua changamoto zinapojitokeza.
Naye, mkazi wa Magomeni, Dar es Salaam, Dickson Peter, aliishauri jamii kujiepusha na matumizi ya fedha yasiyo ya lazima ambayo yatasaidia kuweka akiba itayosaidia kukabiliana na dharura yoyote itakayotokea.
“Kila mwisho wa mwaka huambatana na sikukuu za krisimasi na mwaka mpya, ambazo zinahitaji matumizi mengi ya fedha hivyo, jamii inapaswa kutambua umuhimu wa kuweka akiba kujiepusha na athari za kiuchumi pindi dharura zinapojitokeza.
“Ikumbukwe kuwa, mwaka mpya unapoanza kuna mahitaji muhimu yanahitajika kama ada za watoto shuleni, ulipaji kodi hususan kwa wale waliopanga na mipango endelevu huanza kupangwa mwaka mpya, hivyo jamii inapaswa kutambua kuna akiba husaidia sehemu kubwa ya vitu hivyo.




