REHEMA MAIGALA NA ATHNATH MKIRAMWENI
SERIKALI imesema haitavumilia vitendo vya uvunjifu wa sheria katika usimamizi wa ardhi, hususan jijini Dar es Salaam ambako migogoro, imekuwa ikiongezeka kutokana na baadhi ya watu kuuza ardhi zaidi ya mara moja.
Pia, imesema tayari imeanza mchakato wa kushughulikia tatizo hilo, wizara husika itapitia migogoro yote ya ardhi.
Kauli hiyo, ilitolewa jijini Dar es Salaam jana na Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, katika ziara yake kukagua maendeleo ya ujenzi wa soko na kituo cha mabasi kilichopo Bunju.
Alisema watu wote wanaojua walihusika katika ‘dili’ hizo, wanapaswa kujitokeza mapema kabla serikali haiwachukulia hatua kali.
Alisema haitakuwa tatizo hata kuwafuta kazi wote watakaobainika kuhusika na vitendo hivyo, huku akisisitiza nchi haina uhaba wa watu wa kufanya kazi, isipokuwa inahitaji watumishi waadilifu wanaolinda haki za wananchi na rasilimali za umma.
Alisema kuwa, utaratibu wa watu kutamani ardhi na kuchukua bila kufuata sheria, hauwezi kukubalika na hauwezi kuwa sehemu ya maisha ya taifa.
Dk. Mwigulu alisema yeye kama mkazi wa Dar es Salaam, anaifahamu vizuri changamoto hiyo, amedhamiria kuanza kuishughulikia kikamilifu.
Alisema utekelezaji wa hatua hizo, utafanyika kwa kuzingatia maelekezo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na maagizo yaliyotolewa, yanapaswa kutekelezwa ndani ya siku 40, kurejesha haki, uwajibikaji na nidhamu katika sekta ya ardhi.
WAGENI KUFANYA BIASHARA ZA WAZAWA
Pia, alitoa onyo kwa wafanyabiashara wa kigeni kufanya shughuli hizo ambazo zinaweza kufanywa na Watanzania.
Waziri Mkuu alisema lengo la serikali ni kulinda maslahi ya wananchi na kuhakikisa uchumi wa nchi, unawanufaisha wenyeji.
Dk. Nchemba, alisema sheria zilizopitishwa na Bunge zinahimiza kuwa, biashara zinazoweza kufanywa na Watanzania, raia kutoka mataifa mengine wasifanye.
“Hatutaruhusu wageni kuingia kwenye biashara za wachuuzi wadogo au zile zinazohusisha vijana wa Kitanzania,” alisema.
Alisisitiza kuwa, Wizara ya Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na taasisi zake, zinapaswa kuhakikisha utekelezaji wa sheria hizo, unazingatiwa.
Alisema wafanyabiashara wanapaswa kushirikiana na mamlaka za mitaa, kuhakikisha hawaingizi wageni wasio na vibali sahihi.
Kauli ya Waziri Mkuu inahusisha hali halisi ya baadhi ya hoteli ambako wageni hupangishwa kwa kodi ndogo nao kuwapangisha wengine kwa faida kubwa.
“Mfano mmoja ni pale mpangaji anakusanya dola 5,000, lakini wageni waliopo ndani, wanapangishwa zaidi ya dola 30,000,”alisema
Dk. Nchemba alieleza kuwa hilo ni tatizo kubwa, kwani mipangilio kama hiyo, inachangia kupoteza mapato ya taifa, kudhoofisha wamiliki wa nyumba na kuongeza matatizo ya usalama.
“Tunahitaji kulinda rasilimali zetu na kuhakikisha Watanzania wanapata haki zao kikamilifu,” alisema.
Aidha, serikali imeagiza mamlaka za mitaa, kufuatilia upya mipangilio ya upangaji wa nyumba na hoteli, hivyo wamiliki wanapaswa kushirikiana kuhakikisha wapangaji wao hawaiingizi wageni wasio na vibali.
Waziri Mkuu, alisisitiza Watanzania wanapaswa kupewa nafasi za kwanza katika mikataba ya ununuzi, ujenzi na huduma, hiyo ni sehemu ya kuhakikisha uchumi unakua kwa faida ya wenyeji, siyo wageni.
Dk. Nchemba, alibainisha madhara ya usalama kutokana na wageni kuingia bila udhibiti na kusema hali hiyo, inachangia matatizo yasiyo ya lazima katika jamii na kuathiri ustawi wa wananchi.
“Watanzania wanahimizwa kushirikiana na mamlaka katika kuripoti mipangilio isiyo rasmi, kwani ushirikiano huo, utasaidia kudumisha haki za wenyeji na kulinda rasilimali za taifa.”
Pia, serikali inasisitiza umuhimu wa kodi, ushuru na leseni kufuatwa kikamilifu, hiyo ni njia ya kuhakikisha mapato ya taifa hayapotei kwa faida ya wageni na biashara zinaendelea kwa manufaa ya wananchi.
Dk. Nchemba, alieleza kuwa, serikali inataka kuhakikisha uchumi wa Tanzania unaendeshwa na Watanzania, huku wageni wakiingizwa kwenye fursa ambazo hazina kipingamizi cha kisheria.
Aliwahimiza Watanzania kulinda rasilimali zao, kushirikiana na mamlaka kuhakikisha biashara zinazofanywa nchini, zinawapa manufaa wenyeji.
“Tunatakiwa kuwa na wivu wa taifa letu, kuhakikisha Tanzania ni ya Watanzania na kuzuia shughuli zisizo rasmi za wageni ambazo hazina manufaa kwa wananchi,” alihimiza.
KUKAMATWA KWA KIJANA ALIYEFANYA UTAPELI
Dk. Mwigulu Nchemba, ameviagiza vyombo vya dola, mkoani Arusha, kumkamata kijana aliyedhulumu sh. milioni 600, fedha ambazo alitumia kinyume na malengo ya mkopo aliopatiwa.
Alisema kuwa, kijana huyo alipewa dhamana na familia moja awasaidie kufanikisha mkopo, lakini alitumia fedha hizo kwa manufaa yake binafsi.
“Mama mmoja na mumewe, walimwamini kijana huyo kwa sababu walimjua, wakampa nyaraka muhimu aweze kupata mkopo kwa niaba yao, lakini fedha hazikufika kwa familia hiyo.
“Badala ya kutoa mkopo kwa familia, kijana huyo alikopa sh. milioni 600 kwa niaba yake mwenyewe na hakulipa marejesho, hali iliyosababisha familia ya mama huyo kuanza kudaiwa,” alisema.
Dk. Mwigulu, alisema mama huyo maskini, alianza kushinikizwa, huku mali zake zikichukuliwa nyumbani, licha ya yeye kutokuwa na hatia yoyote.
Waziri Mkuu, alisema hali hiyo haiwezi kukubalika kwani ni kinyume cha sheria na haki kwa mtu asiye na hatia kuteseka wakati mtuhumiwa anatembea huru.
“Haiwezekani mama maskini adaiwe na kupokonywa mali, wakati aliyedhulumu fedha anatembea huru, hilo halitakubalika,” alisema
Kutokana na uzito wa tukio hilo, Mwigulu alimwagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha (RPC), Justine Masejo, kuhakikisha kijana huyo anakamatwa popote alipo na fedha hizo, zirudishwe haraka kwa mhanga.
Pia, alielekeza mali zote za kijana huyo, zichunguzwe na zikamatwe, ikibainika ni matokeo ya utapeli hatua zichukuliwe kwa sababu hakuna aliye juu ya sheria.
Alisema uchunguzi zaidi unahitajika kubaini kama kuna ushiriki wa watumishi wa ndani wa taasisi ya kifedha katika tukio hili.
“Haiwezekani fedha hizi zitoke bila mtu wa ndani kushiriki. Aliyehusika, achukuliwe hatua kali,” alisema.
Aidha, alisisitiza kuwa, mama huyo lazima alindwe, asiteswe na wadai na haki yake ihifadhiwe wakati uchunguzi ukiendelea.
Pia, serikali itahakikisha vitendo vya utapeli havitazidi kuwa kero kwa wananchi maskini na wahalifu wengine wakichukuliwa hatua za kisheria.
Alisema haki lazima itendeke bila kujali hadhi au uhusiano wa mhusika.
Hata hivyo, vyombo vya dola vimeagizwa kufanya uchunguzi wa kina, kumkamata kijana huyo na wengine wanaotuhumiwa na tukio hilo, wachukuliwe hatua za kisheria.




