Na MWANDISHI MAALUMU
WAZIRI Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba, amesisitiza kuwa, serikali itaendelea kushirikiana na viongozi wa dini kujenga taifa lenye hofu ya Mungu, upendo, haki na uwajibikaji.
Dk. Mwigulu alisema hayo, aliposhiriki Ibada ya Jumapili katika Kanisa Kuu Anglikana la Roho Mtakatifu, Dodoma.
“Sote tunatambua kwamba, taasisi za dini zina nafasi ya kipekee ya kuhubiri na kufundisha maadili ya upendo, uvumilivu na kuheshimiana, ambazo ni nguzo kuu za amani ya taifa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, anatambua na kuthamini mchango mkubwa wa taasisi za dini ikiwemo Kanisa la Anglikana, katika kudumisha amani, maadili mema na mshikamano wa kitaifa.
Pia, Mwigulu, alisema kuwa, ibada za Jumapili ni sehemu muhimu ya maisha ya Mkristo, ni muda wa kujitathmini, kuimarisha uhusiano wao na Mungu na kujifunza namna bora ya kuishi kwa mujibu wa mapenzi ya Mungu katika familia, jamii na taifa kwa ujumla.
Alisema Watanzania wanakumbushwa kuishi kwa misingi ya upendo, unyenyekevu, haki na uwajibikaji, kwani Biblia inasisitiza wazi kuwa, “Umejulishwa, ee mwanadamu, yaliyo mema; na Bwana anataka nini kwako, ila kutenda haki, kupenda rehema na kwenda kwa unyenyekevu mbele za Mungu wako,” (Mika 6:8) na maadili hayo si ya kidini pekee, bali msingi muhimu wa ustawi wa jamii na maendeleo ya Taifa.
Dk. Mwigulu, alisema Tanzania imeendelea kuwa kielelezo cha amani, umoja na mshikamano katika ukanda wetu na barani Afrika.
“Amani hii siyo jambo la bahati, bali ni matokeo ya jitihada za pamoja za serikali, taasisi za dini, familia na wananchi kwa ujumla,” alisema.
Waziri Mkuu alisisitiza kuwa, imani wanayojifunza na kuimarisha katika ibada, inapaswa kutafsiriwa katika matendo ya uadilifu, uwajibikaji, bidii kazini, kuheshimu sheria na kushiriki kikamilifu katika kujenga taifa lenye haki, amani na maendeleo endelevu. “Imani ya kweli inapaswa kuonekana kwa matendo.”
Aidha, Dk. Mwigulu alitumia fursa hiyo kutoa wito kwa waumini wote na Watanzania, kuendelea kuwa mabalozi wa amani katika familia zao, maeneo ya kazi na katika jamii kwa ujumla kupinga vitendo vyovyote vya chuki, migawanyiko na vurugu.
Awali, Askofu wa Kanisa Anglikana Tanzania, Dayosisi ya Central Tanganyika, Dk. Dickson Chilongani, aliipongeza serikali kuendelea kushirikiana na taasisi za kidini, likiwemo Kanisa la Anglikana kuhakikisha nchi inaendelea kuwa na amani.
“Tunataka nchi iwe na amani ili shughuli ziendelee na hatutachezea amani,” alisisitiza Waziri Mkuu.




