Na SUPERIUS ERNEST
KATIBU wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Kihongosi, amesema utekelezaji wa ahadi za Chama Cha Mapinduzi (CCM), zilizoahidiwa katika kampeni za Uchaguzi Mkuu kupitia Ilani ya Uchaguzi, zinaendelea kutekelezwa kwa kasi kupitia kauli mbiu; Kazi na Utu, kwa lengo la kuchochea maendeleo ya wananchi na Taifa.
Kihongosi aliyasema hayo, mkoani Singida katika Wilaya ya Manyoni, alipowasalimia mamia ya wannachi, waliojitokeza kumpokea kuanza ziara.
“Nawashukuru sana kwa mapokezi haya makubwa, nitoe salamu za Mwenyekiti wa Chama na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, anajua niko hapa nimeanza ziara hapa Singida.
“Amenipa maneno yafuatayo, niwashukuru kwa kura za kishindo mlizompatia katika uchaguzi mkuu, anawapenda na kuwasaliamia sana.
“Pia, amenambia niwajulishe kuwa Kazi na Utu imeshaanza, kama alivyoahidi katika mikutano yake ya kampeni, kazi kubwa inaendelea kufanyika kwa lengo la kuchochea maendeleo kwa wananchi na Taifa,” alisema.
Aliwasisitiza wananchi wa Manyoni na Singida, kuendelea kudumisha amani na mshikamano wa kukijenga Chama na Taifa, kwani ndiyo msingi wa maendeleo na mafanikio.
Alieleza kuwa, Taifa liko imara kwa sababu ya uongozi thabiti wa CCM, unaoongozwa na Rais Samia.
Alisema ziara yake ilikuwa ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa kwa fedha nyingi zilizotolewa na Serikali ya Rais Samia, hivyo kuangalia kama miradi hiyo imekidhi kiwango cha fedha zilizotolewa.
Katika ziara hiyo, atatumia fursa ya kuzungumza na viongozi wa CCM kuhusu utekelezaji wa miradi hiyo ya maendeleo.
Aliwashukuru sana viongozi wa Mkoa wa Singida na wanachama kwa mapokezi makubwa waliyompa.
Katika hatua nyingine, Kihongosi, alitoa salamu za Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dk. Asha – Rose Migiro, huku akiwaahidi kuwa kiongozi huyo atafika mkoani humo, kutembelea mashina na kuzungumza na wanachama.
Awali, akimkaribisha Kihongosi, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Singida, Martha Mlata, aliwapongeza mamia ya wanachama wa Manyoni kujitokeza kwa wingi kumkaribisha kiongozi huyo.
Mwenyekiti huyo, alisema mvua inanyesha, watu wanalima na chakula cha kutosha kipo mkoani humo, kwa sababu ya uchapakazi wa wananchi.




