Na NASRA KITANA
MAKOCHA Pedro Goncalves wa Yanga na Steve Barker wa Simba wametamba kuwa watashinda katika michezo ya Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya makundi dhidi ya Al Ahly na Esperance De Tunis.
Yanga itashuka nchini Misri kesho kupambana na timu ya Al Ahly katika Uwanja wa Al Salam jijini Cairo kuanzia saa 1:00 usiku.
Kikosi cha Simba kitashuka keshokutwa katika Uwanja wa Stade Olympique Mammadi nchini Tunisia kupambana na Esperance De Tunis ya Tunisia kuanzia saa 1: 00 usiku.
KOCHA WA YANGA
Akizungumza kwa nyakati tofauti Dar es Salaam, jana, muda mfupi kabla ya kuondoka nchini, kocha wa Yanga, Pedro Goncalves alisema uzoefu wa wachezaji wa timu yake, unampa matumaini ya kushinda mchezo huo wa ugenini.
Alisema kuwa kwa sasa timu yake imepata muunganiko mzuri kitu ambacho kitasaidia kuwa bora zaidi na matokeo mazuri.
“Tunakwenda kusaka pointi tatu, natumaini tutazipata, wachezaji wetu hawana presha kwa sababu wamecheza mechi nyingi kubwa. Al Ahly ni timu nzuri na hatari.
“Lakini tumefanya kazi ya kuiangalia na kufahamu jinsi gani tutakwenda kucheza nao katika mechi hii,” alisema.
Pedro alisema kwamba kesho wataingia dimbani katika mchezo huo kwa kuwaheshimu wapinzani wao na kucheza kwa nidhamu kubwa ili kupata matokeo.
KOCHA WA SIMBA
Kocha wa Simba, Steve Barker alisema wanaenda kucheza mchezo ambapo wameweka mkakati’ kushinda dhidi ya wenyeji Esperance De Tunis.
Barker alifafanua kuwa wanakwenda kucheza mechi hiyo kwa uangalifu mkubwa kwa sababu wanahitaji kumaliza dakika 90 kwa kupata pointi tatu ambazo ni muhimu.
“Itakuwa ni mechi ngumu na ya tofauti sana, tunakwenda kucheza na timu ambayo ni nzuri sana ikiwa nyumbani kwao, tutapambana mwanzo mwisho kuhakikisha tunapata matokeo mazuri na kutinga robo fainali,” alisema Barker.
Kocha huyo alisema wachezaji wake wanatakiwa kuwa makini, hasa wakiwa na mpira na kipindi ambacho hawana mpira.
MSIMAMO
Katika msimamo wa michuano hiyo, timu ya Yanga ipo nafasi ya pili katika kundi B ikiwa na pointi nne sawa na Al Ahly inayoongoza kundi zikicheza mechi mbili.
Kwa upande wa Simba ikiburuza mkia katika kundi D, haijashinda mchezo wowote huku Esperance ikiwa na pointi mbili ikipata sare katika mechi mbili za awali na kushika nafasi ya tatu.




