Na MWANDISHI WETU
HATMA ya uongozi wa Mwenyekiti wa klabu ya Simba,chini ya Murtaza Mangungu itajulikana baada ya mechi yao dhidi ya Petro Atletico ya Luanda nchini Angola.
Simba itashuka dimbani keshokutwa kupambana na Petro katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL) hatua ya makundi,mchezo utaofanyika saa 1:00 usiku.
Taarifa iliyopatikana Dar es Salaam, imeeleza kuwa uongozi wa Chama Cha Soka Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) unasubiri viongozi wa klabu hiyo warudi nchini ndio mchakato wa Uchaguzi Mkuu uanze.
“Mambo yote yanakwenda vizuri DRFA tunasubiri viongozi wa Simba wakimaliza mchezo huo, tukae nao tujue mchakato mzima utakuwaje,”alisema mtoa taarifa hiyo.
Chanzo hicho, kimeeleza kwamba, kazi hiyo itafanyika kwa kufuata maelekezo ya Kamati ya Uchaguzi ya DRFA na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania(TFF).
Juhudi za kuwapa viongozi wa DRFA kuzungumza jambo hilo, zilishindikana.
Aidha, gazeti hili, lilimtafuta Msajili wa Vyama Vya Michezo Tanzania, Abel Ngilangwa ambaye alisema hana taarifa juu ya uchaguzi huo.
“Sina taarifa yoyote kwa sababu sijapata barua hivyo mnapaswa kuwasiliana na DRFA au Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ambao ndiyo wahusika wa kwanza.
“Lakini kwa upande wa huku kwetu ni mbali sana, pia sisi tunafahamu DRFA wao wanatakiwa watupe taarifa juu ya uchaguzi wa klabu ya Simba,”alisema kiongozi huyo.
Hadi sasa, klabu hiyo inaongozwa na Mangungu ambaye alichaguliwa Mwenyekiti katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Februari 7, mwaka 2021.
Katika uchaguzi huo Mangungu alipata kura 802 huku mpinzani wake, Juma Nkamia alipata kura 330 kati ya kura 1140 zilizopigwa na wanachama wa Simba.
Hatua hiyo, inakuja baada ya kuwepo taarifa kwamba uongozi wa sasa wa klabu chini ya Mangugu muda wao wa kuongoza ulimalizika Januari 12, mwaka huu.
Lakini mwishoni mwa wiki mara baada ya mchezo kati ya Simba na Esperance ya Tunisia kumalizika kwa kufungana 2-2, baadhi ya mashabiki wa klabu hiyo walimvamia Mangungu na kumfanyia fujo.
Simba ipo kundi D linaongozwa na Stade Malien yenye pointi nane ikifuatiwa na Esperance yenye pointi sita huku Petro Luanda ikiwa na pointi tano na Simba ina pointi moja.
Tukio hilo, lilitokea wakati Mangungu alipokuwa anatoka jukwaani kuelekea katika gari lake lililokuwa katika maegesho ya Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Hali hiyo, ilisababisha askari wa Jeshi la Polisi kumuondoa kiongozi huyo chini ya ulinzi mkali.
Mashabiki hao walisikika wakieleza kwamba hawamtaki kiongozi huyo na kumshinikiza atangaze kujiuzulu.
BODI YA SIMBA
Awali Bodi ya Wakurugenzi wa klablu hiyo, ilitoa taarifa ya kusikitishwa na vitendo vya baadhi ya watu kumvamia na kumfanyia fujo mwenyekiti huyo baada ya kumalizika kwa mchezo wao.
Taarifa hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, Crescentius Magori ilieleza kuwa klabu hiyo imelaani tukio hilo na kutaka wahusika wachukuliwe hatua.
“Bodi ya Wakurugenzi ya Simba imesikitishwa na vitendo vya baadhi ya watu kumvamia na kumfanyia fujo Mwenyekiti wa Klabu na Makamu Mwenyekiti wa Bodi, Mangungu baada ya mchezo wetu dhidi ya ES Tunis kumalizika katika Uwanja wa Benjamin Mkapa.
“Vitendo hivyo sivyo vya kiungwana, havikubaliki na havitafumbiwa macho, Uongozi wa Klabu unatoa pole kwa Mwenyekiti Mangungu kwa kadhia hiyo.
Aidha taarifa hiyo ilieleza kwamba uongozi wa klabu hiyo, umeliandikia Jeshi la Polisi kuchukua hatua za kisheria kwa wote waliohusika katika vurugu hizo au kula njama ili kuwafikisha katika vyombo vya sheria.
Bodi ilisisitiza kuwa haitabariki wala kuvumilia mtu yoyote atakayeharibu taswira ya klabu kwa namna yoyote.
Sare hiyo ya mabao 2-2 ambayo Simba imepata leo, imeifanya iwe timu ya kwanza kuaga hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu huu ikiwa na pointi moja.
Hii ni mara ya pili kwa Simba kuishia hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika ambapo mara ya kwanza ilikuwa ni 2003.
MANGUNGU
Mangungu alivunja ukimya na kueleza kwamba hatowachukulia hatua yeyote mashabiki ambao walimfanyia fujo.
“Kiukweli mimi sijaona vurugu yeyote ile kule ni kutoelewana na mashabiki na mimi kama mwenyekiti wao siwezi kuchukua hatua yeyote ile kwa mashabiki hao,” alisema Mangungu.
Mwenyekiti huyo alisema kwa sasa mashabiki na wapenzi wa Simba wanatakiwa kuwa watulivu ili timu yao iweze kurudi katika mstari na kufanya vizuri kama ilivyokuwa zamani.




