Na LILIAN JOEL, Arusha
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba amemwagiza Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dk. Toba Nguvila na Mkurugenzi wa Jiji la Arusha, John Kayombo kukaa na Benki ya CRDB na wadau wa sekta binafsi kutafuta fedha za ujenzi wa Mradi wa Mabasi yaendayo Haraka (BRT), yatakayotumia gesi wakati wa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027.
Michuano ya AFCON 2027, inatarajiwa kufanyika katika nchi za Tanzania, Kenya na Uganda.
Aidha, amemwagiza Kayombo kutenga maeneo ya akiba kwa upanuzi wa stendi kuu ya kisasa ya Mkoa wa Arusha, yatunzwe na kulindwa yasivamiwe kuepuka migogoro isiyo na tija.
Waziri Mkuu alitoa maagizo hayo jijini Arusha, alipokagua maendeleo ya ujenzi wa Stendi Kuu ya Mabasi inayojengwa katika eneo la Bondeni City, Arusha.
Dk. Mwigulu aliagiza makadirio ya muda wa nyongeza yafanyike haraka ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kuanza kutoa huduma kwa wananchi.
“Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dk. Toba Nguvila pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha, John Kayombo nendeni mkakae na Benki ya CRDB ambayo ina fedha za mazingira (Green Fund) sanjari na wadau wengine ili mjenge mradi wa BRT katika kuelekea mashindano ya AFCON 2027,” alisema Waziri Mkuu.
Aidha, Dk. Mwigulu ameagiza kuharakishwa kwa ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya barabara zinazoelekea katika maeneo muhimu ya mashindano hayo, ikiwemo barabara ya kutoka ‘By Pass’- Kikwe–Mirerani hadi Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) ili kuhakikisha wageni na washiriki katika mashindano hayo wanapata huduma bora za usafiri.
“Arusha ni jiji la kimkakati kwa shughuli za utalii na biashara, maandalizi ya miundombinu hasa ya barabara ni muhimu hasa kuelekea mashindano ya AFCON 2027 yanayotarajiwa kufanyika hapa nchini ikiwemo Jiji la Arusha mwakani,” alisema.
Waziri Mkuu alisisitiza kuwa Arusha inapaswa kwenda sambamba na hadhi ya majiji mengine yatakayokuwa wenyeji wa mashindano ya AFCON 2027, ikiwemo Dar es Salaam na Zanzibar kwa kuboresha miundombinu na huduma za kijamii.
Alieleza kuwa mradi huo ni zawadi kubwa kutoka kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa wananchi wa mkoa wa Arusha, akitambua kuwa stendi ya hivi sasa imekuwa kero kutokana na msongamano mkubwa wa magari na wafanyabiashara.
MKURUGENZI ATOA NENO
Awali akiwasilisha taarifa ya ujenzi huo wa stendi, Kayombo alisema unatekelezwa na serikali ya awamu ya sita kwa gharama ya sh. bilioni 14.3 kwa ufadhili wa Benki ya Dunia ikiwa ni sehemu ya miradi ya kimkakati katika majiji yote nchini.
“Lengo la mradi huu ni kuboresha mazingira ya usafiri kwa abiria wanaoingia na kutoka katika Jiji la Arusha ambao unajumuisha jengo kuu la mabasi lenye ghorofa lenye sehemu za kusubiri usafiri, maduka 23.
“Pia kutakuwa na maeneo mawili ya wafanyabiashara wa vyakula, vyoo vya kisasa, nyumba ya walinzi, vituo vya ukaguzi, vituo vya kukusanyia taka na sehemu ya kukutania wakati wa dharura,” alisema.
Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Paul Makonda, alisema mradi huo ni utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na utatoa fursa kubwa kwa wafanyabiashara pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa jiji hilo.




