Na MWANDISHI WETU
WAZIRI wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, amesema serikali kupitia taasisi zake inaendelea kuboresha na kuimarisha miundombinu ya usafiri na huduma za uokoaji majini ili kulinda usalama wa wananchi na mali zao na kuchochea maendeleo ya uchumi wa taifa.
Waziri Mbarawa, ametoa kauli hiyo jijini Dar es salaam aliposhiriki futari iliyoandaliwa na Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania-TASAC, iliyowakutanisha wadau wa sekta ya usafiri majini kwa ili kuimarisha ushirikiano na kujadili mustakabali wa sekta hiyo.
Amewahimiza wadau wa sekta ya usafiri majini kushirikiana na Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kuwa salama, yenye ufanisi na inayotoa mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa nchi.
Aidha, Waziri Mbarawa, ameipongeza TASAC kwa kuendelea kusimamia na kudhibiti shughuli za usafiri majini nchini kwa ufanisi, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha usalama wa vyombo vya majini, kulinda mazingira ya bahari na maziwa, pamoja na kusimamia utekelezaji wa sheria na mikataba ya kimataifa inayohusu usafiri majini.
Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, inaendelea kuweka mkazo katika kuimarisha miundombinu ya uchukuzi pamoja na usimamizi wa sekta mbalimbali ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Naye, Mkurugenzi Mkuu wa TASAC, Mohamed Salum, amesema hafla hiyo ya futari imelenga kuimarisha mshikamano, kujenga mahusiano imara na kuthamini ushirikiano uliopo kati ya TASAC na wadau wa sekta ya usafiri majini.
Kupitia ushirikiano huo, amesema wadau wataendelea kufanya kazi kwa pamoja kuhakikisha sekta ya usafiri majini inakuwa salama, yenye tija na inachangia kikamilifu katika maendeleo ya taifa.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TASAC, Mussa Mandia, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali, taasisi zake na wadau wa sekta binafsi katika kuendeleza sekta ya usafiri majini na kuhakikisha inakuwa salama, yenye ufanisi na yenye mchango mkubwa katika uchumi wa taifa.




