Na MWANDISHI WETU
WAZIRI wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema Tanzania ina mtandao mkubwa zaidi wa barabara kulinganisha na nchi yoyote ukanda wa Afrika Mashariki.
Pia, Ulega amesifu jitihada za Watanzania kujenga taifa lao kwa nguvu na maarifa yao.
Akizungumza Dar es Salaam, Ulega alisema kwa ujumla Tanzania ina mtandao wa barabara wenye urefu wa kilometa 182,000 ambapo kilometa 16,000 zikiwa za lami.
Ingawa hakutaja mtu au tukio lolote, maelezo ya Ulega ni kama majibu dhidi ya madai yaliyotolewa juzi na Rais wa Kenya, William Ruto.
Rais Ruto, alidai Kenya ina mtandao mkubwa zaidi wa barabara za lami, ukilinganisha na nchi nyingine jirani.
“Wenzetu wamesema wana kilometa 20,000 za lami. Na wanasema kiwango hicho ni kikubwa kuliko barabara za lami zote zilizopo katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC). Hata hivyo, sisi peke yetu tuna kilometa 16,000. Jirani zetu Uganda wana kilometa 6,100.
“Ukijumlisha kilometa za lami za Tanzania na Uganda, tayari unakuwa umevuka kiwango cha lami cha Kenya. Kwa hiyo, zile takwimu kuhusu sisi na wenzetu wa Afrika Mashariki hazikuwa sahihi,” alisema Ulega.
Akitoa taarifa zaidi, Ulega alisema kuna mtandao wa kilometa 5,100 ambazo zinajengwa nchi nzima na kuna mikataba ya ujenzi wa kilometa 3,700 za lami, ambazo zimesainiwa, zinasubiri kuanza ujenzi wake.
“Jambo zuri zaidi kuhusu Tanzania wakati tunapata Uhuru, tulikuwa na kilometa za lami zisizozidi 600. Zaidi ya kilometa 15,000 tumezijenga wenyewe kwa nguvu zetu.
“Kuna jirani zetu walikuta wakoloni wamewajengea maelfu ya kilometa za barabara. Sisi waasisi wetu walijua hatuna mjomba wala shangazi wa kutujengea, na tumefanya tulichofanya kwa nguvu na maarifa yetu wenyewe, alisema Ulega.
Juzi, Rais Ruto alitumia takwimu za barabara Kenya, akijaribu kujenga hoja kwanini bei ya mafuta nchini kwake ni kubwa kuliko Tanzania, ingawa nchi zote mbili zina bandari.
“Bei ya mafuta Kenya, inaakisi ukweli tunahudumia mtandao mkubwa zaidi wa barabara za lami kuliko nchi zote za jirani ukiziunganisha kwa pamoja. Sisi tuna mtandao mkubwa zaidi kuliko wengine.
“Zaidi ya kilometa 20,000 tulizonazo, tunajenga kilometa nyingine za lami 6,000. Nchi nyingine zimetumia miaka 60 kujenga kilometa 6,000 za lami.”
Ulega alizungumza hayo jijini Dar es Salaam jana, katika tukio la kusainiwa mkataba wa ujenzi wa miundombinu ya Bonde la Mto Msimbazi.



