Na MWANDISHI WETU
KAMPUNI ya Taifa Gas Tanzania Limited inayomilikiwa na mfanyabiashara Rostam Aziz, imeingia makubaliano ya kununua sehemu ya hisa katika biashara ya gesi ya Orca Energy Group Inc. nchini Tanzania, hatua inayotajwa kuwa ya kihistoria katika sekta ya nishati.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Aprili 13, 2026, Taifa Gas itanunua asilimia 49 ya hisa za kampuni ya PAE PanAfrican Energy Corporation (PAEM), huku kampuni ya Amber Energy Investment L.L.C-FZ ikichukua asilimia 51 iliyobaki.
Makubaliano hayo yanahusisha uuzaji wa asilimia 100 ya biashara ya Orca nchini Tanzania, ikiwemo haki zake zote katika mradi wa gesi wa Songo Songo, ambao ni mhimili muhimu wa uzalishaji wa gesi kwa matumizi ya umeme na viwanda.
Hatua hiyo inatajwa kuwa sehemu ya mabadiliko makubwa ya umiliki katika sekta ya gesi, ambapo wawekezaji wa ndani wanaanza kuchukua nafasi kubwa zaidi katika rasilimali za kimkakati.
Akizungumzia maendeleo hayo, Rostam alisema mpango huo umechukua muda mrefu kuandaliwa na unalenga kuhakikisha Tanzania inanufaika zaidi na rasilimali zake za asili.
Alisema kuongezeka kwa umiliki wa Watanzania kutasaidia kuimarisha uchumi wa ndani na kuongeza uwekezaji katika sekta ya viwanda inayotegemea nishati ya gesi.
Aidha, alibainisha kuwa mradi wa Songo Songo umechangia kwa kiasi kikubwa mapato ya serikali, ajira na maendeleo ya ujuzi kwa Watanzania.
Kwa upande wake, Orca imeeleza kuwa uamuzi wa kuuza biashara yake umetokana na tathmini ya kina ya changamoto za uendeshaji nchini.
Kutokana na hali hiyo, Orca imeona ni busara kuuza biashara hiyo ili kulinda maslahi ya wanahisa wake.
Shughuli za Orca nchini zilikuwa zinaendeshwa kupitia kampuni ya PanAfrican Energy Tanzania Limited, ambayo inashikilia haki na wajibu katika makubaliano ya uzalishaji gesi kati yake, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na Serikali.
Baada ya kukamilika kwa mauzo hayo, Orca haitakuwa tena na umiliki wowote katika biashara yake ya Tanzania wala wajibu wowote unaohusiana na shughuli hizo.
Hata hivyo, kukamilika kwa makubaliano hayo kunategemea kupatikana kwa idhini za kisheria kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Tume ya Ushindani na Waziri mwenye dhamana ya mafuta.
Wachambuzi wa masuala ya nishati wanasema hatua hiyo inaweza kuongeza ushiriki wa wazawa, kuimarisha ushindani na kufungua ukurasa mpya wa maendeleo ya sekta ya gesi nchini Tanzania.




