Na AMINA KASHEBA
WALIMBWENDE kutoka zaidi ya nchi 130 duniani wanatarajiwa kuipamba Tanzania watakapochuana katika mashindano ya ‘Miss World’ yatakayofanyika mwakani.
Mashindano hayo makubwa ya urembo duniani yatafanyika nchini kwa mara ya kwanza huku serikali ikijidhatiti kufanya maandalizi ya kutosha kuhakikisha hafla hiyo inabamba.
Hayo yalisemwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda jijini Dar es Salaam katika hafla ya utiaji saini wa uenyeji wa mashindano hayo yatakayofanyika mwakani nchini.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na watu mbalimbali wakiwemo warembo wa dunia wakiongozwa na Opal Suchata (Miss World), Hasset Dereje (Miss World Africa 2025) na Latricia Ian ambaye ni Miss World Tanzania 2026.
“Serikali tuna mpango wa kuandaa mashindano haya mara mbili au tatu mfululizo kwa sababu tumeona baadhi ya nchi zimeandaa mara nyingi kama Afrika Kusini wameandaa mara nne.
“Tukio hili linakwenda kuweka historia kubwa kwani Tanzania tunakwenda kuwa mwenyeji wa mashindano ya Miss World ya 74, tunaweka historia kwa ukanda wa Afrika ni nchi ya pili ilianza Afrika Kusini na Afrika Mashariki tunakuwa wa kwanza,” alisema.
Makonda alisema kuwa mwenyeji wa mashindano hayo kunalenga kuitangaza Tanzania kimataifa na kukuza sekta za utalii, sanaa na michezo.
“Mbali ya mashindano ya AFCON kufanyika Tanzania mwakani tutakuwa na tukio lingine kubwa la Miss World, hatua hii itafanya nchi kuwa kitovu cha matukio ya kimataifa, hii ni fursa kwa Watanzania kwani tunakwenda kuiweka nchi duniani.
“Kwani mashindano haya yanatazamwa na watu wengi duniani, zaidi ya bilioni mbili hivyo ni muda wa Watanzania kutumia fursa hii muhimu, kwa sababu sekta ya urembo inabeba ajira nyingi kwa vijana ikiwemo wapambaji kucha,” alisema.
Naye Mkurugenzi wa Miss World, Julia Morley, alisema mashindano hayo yataleta faida kubwa kwa Tanzania ikiwemo kukua kwa utalii nchini kutokana na idadi ya nchi ambazo zitashiriki.
“Mashindano haya yatashirikisha nchi 130, kutakuwa na wageni zaidi ya 200 hivyo Tanzania itapata fursa ya kukuza utalii wao, pia itajitangaza na kufahamika kutokana na televisheni zaidi ya 100 zitakuwa zinaonyesha tukio hili,” alisema.
Aliongezea kuwa, mashindano hayo yatadumu zaidi ya siku 28 kutokana na uwepo wa mashindano madogo madogo ambayo warembo watashiriki kabla ya kuingia fainali.







