Na MWANDISHI WETU
KIUNGO nyota wa Yanga, Mudathir Yahya, anatarajiwa kuukosa mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Simba utakaopigwa Mei 3, mwaka huu jijini Dar es Salaam.
Mudathir ataukosa mtanange huo kufuatia jana Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPLB), kumfungia kucheza mechi tatu na faini ya sh. milioni moja kwa kosa la kumpiga kiwiko mchezaji wa Pamba Jiji, Ibrahim Abraham katika mechi ya ligi hiyo iliyopigwa hivi karibuni katika Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na TPLB, adhabu hiyo imetokana na kanuni ya 14.5 (5.2) ya ligi kuhusu udhibiti wa wachezaji.
Aidha, kamati hiyo iliitoza klabu ya Simba faini ya sh. milioni 10 kwa kosa la shabiki wa timu hiyo kumrushia chupa ya maji mwamuzi msaidizi namba mbili baada ya kunyoosha kibendera kuashiria mchezaji wa Simba kuotea katika mtanange dhidi ya Azam FC.
“Klabu ya Azam FC imetozwa faini ya sh. milioni tano kwa kosa la viongozi wa benchi la ufundi pamoja na wachezaji kutumia mlango usio rasmi wa kuingia uwanjani kinyume na matakwa ya kanuni ya 17:21 ya ligi.
“TRA United na Simba zimetozwa shilingi milioni tano kila moja kwa kosa la walinzi wa klabu hizo (Stewards) kupigana mara baada ya ya timu hizo kuwasili katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mkoani Arusha, “ ilieleza.
“Vilevile klabu ya Singida Black Stars ya mkoani Singida imetozwa sh. milioni tano kwa kosa la viongozi wake wawili kuingia uwanjani na kumwaga vimiminika, viongozi hao walifanya tukio hilo lililotafsiriwa kama kitendo vinavyoashiria imani za kishirikina,” ilieleza taarifa hiyo.



