Na MWANDISHI WETU
WAKATI Ligi Kuu Tanzania Bara ikisimama kupisha Kombe la Muungano 2026, takwimu zinaonyesha kuwa timu nne zinaongoza kuwa na safu butu ya ushambuliaji katika michuano hiyo.
Katika ligi hiyo, hadi sasa kila timu imeshacheza mechi 19, ambapo baadhi zinawania ubingwa huku nyingine zikipigania kutoshuka daraja.
Kwa mujibu wa msimamo wa liigi hiyo, timu nne ambazo zina safu butu ya ushambuliaji hadi sasa msimu huu ni KMC iliyofunga mabao manane, Tanzania Prisons mabao 10 sawa na Fountain Gate na Mashujaa.
Timu hizo zinafuatiwa na Mbeya City, Coastal Union na Mtibwa Sugar ambapo kila moja imefunga mabao 16 katika mitanange 19 iliyocheza.
Namungo inafuatia kwa timu zilizopachika mabao machache zaidi ikiwa imefunga mabao 17, Dodoma Jiji imepachika mabao 18 na Pamba Jiji imefunga mabao 19.
Zilizofunga mabao 20 ni TRA United na JKT Tanzania wakati Singida Black Stars ikiweka kimiani mabao 21.
Wakati Azam FC ikifunga mabao 26, Yanga ndiyo kinara wa upachikaji wa mabao baada ya kufunga mabao 44 huku Simba ikifunga mabao 32.



