Mwandishi Wetu
BAADA ya kuwasilishwa ripoti ya vurugu za Oktoba 29, 2025, wadau wa siasa na diplomasia, wamesema mustakabali wa taifa unahitaji kufuata njia ya maridhiano, kurejesha imani ya wananchi na kuimarisha utulivu.
Wakati wadau wakieleza hayo, serikali imesema hatua iliyochukua siku ya ghasia za Oktoba 29, 2025 ni kuwalinda raia wake, ikisisitiza kila hatua ililenga kuwalinda raia na kurejesha amani.
Wachambuzi wa siasa walisema baada ya kutolewa ripoti ya Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, hivi sasa Watanzania wanatakiwa kuungana na kukaa katika meza ya maridhiano.
Walisema kwa muda mrefu Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amekuwa tayari kwa mariadhino lengo ni kuendelea kuliunganisha taifa hivyo, ni muda mwafaka kwa wadau wote kumuunga mkono.
Kauli za wadau hao zimetolewa siku chache baada ya Tume hiyo iliyokuwa chini ya Jaji Mohamed Chande, kuwasilisha na kukabidhi ripoti yake kwa Rais Dk. Samia.
Miongoni mwa mapendekezo, Tume hiyo ilishauri kuanzishwa Tume ya Mariadhiano chini ya mamlaka ya Rais ili kuhakikisha vurugu kama hizo hazijirudii tena nchini.
Akihojiwa na vyombo vya habari vya kimataifa, Mshauri wa Rais wa Diplomasia, Balozi Lazaro Nyalandu, alisema siku zote serikali iko mstari wa mbele kulinda wananchi wake na kauli ya Rais Dk. Samia inadhihirisha utayari wa serikali kuwalinda wananchi.
Alisema Tume ya Jaji Chande imewasilisha taarifa yake huku akieleza ukweli wa baadhi ya mambo yaliyokuwa yakilitatiza taifa yamewekwa hadharani, ikiwemo hatua zilizochukuliwa na serikali.
Pia, Balozi Nyalandu alisema Tume imeeleza na kuweka ushahidi namna baadhi ya waandamanaji walioingia barabarani wakiwa na silaha kama bunduki na vilipuzi, ikiwemo kupatiwa mafunzo kwenye kambi mbalimbali ili kutekeleza vurugu hizo.
“Kama ilivyoeleza Tume kwenye ripoti yake, kwa sababu kilichotokea Oktoba 29, 2025 ilikuwa ni matukio ya kupangwa, Serikali ilichukua hatua ya kuokoa maisha ya watu. Ilikuwa siku ngumu kwa kila Mtanzania,” alisema Balozi Nyalandu.
Hata hivyo, alisisitiza Watanzania wanapaswa kumuunga mkono Rais Dk. Samia kutekeleza alichoahidi wakati akipokea ripoti hiyo.
Rais Dk. Samia aliahidi watu waliopata majeraha na wanaoendelea na matibabu na kuhitaji vifaa vya usaidizi, serikali itasimamia na itakuwa bure.
Pia, aliahidi kuunda chombo kuchunguza vitendo vyote vya jinai, huku akisisitiza uwajibikaji kwa watakaobainika kuhusika na hatua zaidi.
Kuhusu uhalali wa Tume ya Jaji Chande, Balozi Nyalandu, alisema iliongozwa na watu wenye weledi na uzoefu mkubwa ndani na nje ya Tanzania na uwasilishaji wa ripoti yake ulikuwa wa wazi.
“Hii tume ilikuwa na watu waliowahi kushika nyadhifa kubwa ndani na nje ya Tanzania. Nashangaa wanaohoji uhalali wake wanaangalia vigezo gani. Mchakato wake ulikuwa wazi sana na ulihusisha wadau mbalimbali, wakiwemo wa vyama vya siasa
“Jambo la msingi Watanzania wote kuungana kwa dhati na kuaminiana ili tuendelee kuijenga Tanzania. Tukae kwenye meza za mazungumzo kwa maslahi mapana ya kizazi cha sasa na kijacho. Rais Samia siku zote amekuwa na dhamira ya dhati ya kuhakikisha Watanzania wanakuwa wamoja na wanapata haki sawa. Hili linadhihirishwa na utekelezaji wa falsafa ya 4R tangu ameshika madaraka mwaka 2021,” alisema Balozi Nyalandu.
Kwa upande wake mchambuzi wa siasa nchini, Dk. Baraka Mfinanga, alisema taifa lolote linalopitia mtikisiko wa kisiasa, linaweza kutumia kipindi hicho kujenga mkataba mpya wa kijamii badala ya kubaki katika lawama.
Alisema maridhiano yasiyoambatana na mageuzi ya taasisi, hubaki kuwa mapatano ya muda mfupi, lakini yanapojengwa juu ya maboresho huleta utulivu wa kudumu.
Dk. Mfinanga, alisema kuimarisha mifumo ya uchaguzi, kuendeleza mazungumzo ya kisiasa na kufungua ushiriki wa vijana ni hatua muhimu zinazopaswa kuchukuliwa.
Mchambuzi wa majanga, Dk. Neema Kasesela, alisema hoja ya maridhiano haiwezi kutenganishwa na imani ya wananchi kwa taasisi, akieleza ndiyo mtaji mkuu wa utulivu wa muda mrefu.
Alisema mjadala wa Katiba, haki na uwajibikaji haupaswi kutazamwa kama chanzo cha mgawanyiko, bali kama sehemu ya kuijenga upya misingi ya uaminifu wa taifa na Rais ameahidi kutimiza.
Dk. Kasesela alisema nafasi ya vijana ni muhimu pia kuzingatiwa, kwa kuwa kundi hilo lina mchango mkubwa katika mustakabali wa kisiasa, kiuchumi na kijamii.




