Na MWANDISHI WETU
JASHO limemwagika. Ndivyo unavyoweza kusema baada ya timu za Simba na Yanga jana kutoka sare ya mabao 2-2 katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Katika mtanange huo uliopigwa Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam, watani hao wa jadi walionyesha burudani ya aina yake iliyotawaliwa na magoli manne mazuri.
Simba ilikuwa ya kwanza kutangulia kwa mabao 2-0 ndani ya dakika 10 za mchezo kabla ya Yanga kurudi mchezoni na kusawazisha mabao hayo.
Wekundu hao wa Msimbazi walipata bao la kwanza dakika ya tatu kupitia Libasse Gueye aliyeunganisha kwa mguu wa kushoto pasi mahiri kutoka kwa Clatous Chama.
Dakika saba baadaye, Simba ilipata bao la pili lililofungwa na Chama aliyeweka mpira kimiani kwa ‘tiki taka’ akiunganisha pasi ya juu iliyopigwa na Ellie Mpanzu. Dakika ya 18, Yanga ilirejea mchezoni kwa bao la Prince Dube aliyefunga kwa mguu wa kulia akipokea pasi ya Duke Abuya.
Dakika ya 51, Bakari Mwamnyeto aliifungia Yanga bao la kusawazisha kwa mguu baada ya kichwa cha Dube kuokolewa na kipa Kassali.
Kutokana na matokeo hayo, Yanga inaendelea kuongoza ligi ikiwa na pointi 48 katika mechi 20 ikifuatiwa na Simba yenye pointi 43 katika mechi 20, kila timu ikiwa na mechi 10.



