Na ZIANA BAKARI
BAADHI ya wadau wakiwemo, wasomi na wachumi wamepongeza kauli ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ya kutoa onyo kali kwa watu wote wanaojaribu kuvuruga amani ya nchi.
Pongezi hizo zilitolewa baada ya Rais Dk. Samia kusisitiza watu hao kuacha mara moja kwa sababu, vitendo hivyo ni hatari kwa mustakabali wa taifa, huku akibainisha kuwa, serikali itashirikiana na wananchi kuhakikisha mazingira ya uwekezaji yanakuwa rafiki na amani ikilindwa.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na UHURU, baadhi ya wadau hao, walisema amani ikiwepo, itasaidia sehemu kubwa ya wawekezaji kuja kuwekeza nchini na uchumi kukua.
DK. MAGUO
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Dk. Mohamed Maguo, alisema anaunga mkono kauli hiyo ya Rais Samia kwa kuwa, amani ni msingi wa kila kitu.
Alisema sehemu yoyote yenye amani, huvutiwa zaidi wawekezaji kuja kuwekeza, alihimiza amani izidi kuendelea kuwepo nchini.
“Mtu hawezi kuleta teknolojia yake sehemu ambayo haina amani, tunapaswa kujua kuwa, uwekezaji unapofanyika, unasaidia kuchochea ajira mbalimbali na uchumi kukua.
“Niwaombe sana wananchi tuendelee kulinda amani ya nchi yetu izidi kuonekana kisiwa cha amani, tusikubali kushawishika na mtu yoyote na kuvuruga amani ya nchi yetu,”alisema.
DK. RUGEIHYAMU
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk. Sylvester Rugeihyamu, alisema suala la amani ndani ya nchi, linapaswa kuzingatiwa na kila mtu.
Alifafanua kuwa, amani ikiwepo husaidia kuleta maendeleo na mwananchi kuwa huru kuendelea na shughuli zao za kila siku bila hofu yoyote.
“Tunapaswa kulinda amani kwa vitendo zaidi, tuwe wazalendo wa kupenda taifa letu, naunga mkono kauli ya Rais Samia, nampongeza kwa hilo,”alisema.
Dk. LYANGA
Mhadhiri wa Uchumi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Dk. Timothy Lyanga, aliwapongeza viongozi kuendelea kusisitiza suala la amani ndani ya nchi.
Akizungumzia umuhimu wa amani, Dk. Lyanga, alisema utasaidia upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi na maendeleo ya kiuchumi.
“Hali ya amani inapokuwepo, huwezesha maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kiutamaduni kwa sababu, kwa kuwa inawapa watu uhuru wa kufanya shughuli zao za kila siku bila ya wasiwasi na tuendelee kuwasikiliza viongozi wetu wanachotusihi,” alisema.
Dk. MMARI
Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti, Sera na Uchumi (REPOA), Dk. Donald Mmari, alisema kila kitu hakiwezi kufanyika bila ya uwepo wa utulivu.
Alisema suala la amani, upendo na ushirikiano, vinapaswa kupewa kipaumbele kwa kuwa, vinasaidia kuwaweka watu kuwa wamoja.
“Niwasihi wananchi tupendane na tuipende nchi yetu, tusikubali kuhatarisha amani ya nchi yetu, tushirikiane katika kila jambo tunalolifanya, naamini Mwenyezi Mungu atatusimamia,”alisema.
Januari 9, mwaka huu, Rais Dk. Samia alisema amani na utulivu wa kisiasa ni nguzo muhimu kwa maendeleo ya uchumi na ustawi wa wananchi.
Rais Dk. Samia aliyasema hayo alipozindua Hoteli ya Jaz Elite Aurora iliyopo eneo la Michamvi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.
Alisema amani ni chanzo cha ukuaji wa sekta ya utalii, ambayo imeendelea kuchangia kwa kiasi kikubwa pato la taifa.
“Kwa hiyo amani ikivunjika haichagui, niwaombe sana, maendeleo yetu, kunawiri kwetu, kupendeza kwetu, kulala na kuamka salama, tutunze amani ya nchi yetu, tofauti za mawazo zipo, lakini zisitugawe wala tusiharibu utulivu wa kisiasa na amani ya nchi yetu,”alisema.




