REHEMA MAIGALA na ATHNATH MKIRAMWENI
ZIARA ya Rais wa Kenya, William Ruto, nchini na hatua ya kusainiwa mikataba minane ya ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili, imeibua matumaini mapya kwa wadau wa uchumi huku wakieleza mitazamo yao.
Pia, wataalamu hao, walieleza kuwa, uamuzi wa kuondoa vikwazo visivyo vya kikodi, utafungua ukurasa mpya wa biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo.
Walisema kuwa, hatua hiyo ni ishara ya kuimarika kwa uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi, jambo litakalorahisisha usafirishaji wa bidhaa, kuongeza fursa za masoko na kuchochea ukuaji wa shughuli za uzalishaji mali katika ukanda wa Afrika Mashariki.
PROFESA WANGWE
Akizungumza na gazeti hili jana, mtaalamu wa uchumi nchini, Profesa Samuel Wangwe, alisema makubaliano yaliyopo kati ya nchi hizo, yametokana na uhusiano mzuri kati yake.
Alisema uhusiano huo, utasaidia kuimarisha uchumi wa nchi na kujenga urafiki mzuri unaotokana na kuwepo diplomasia ya kweli.
Profesa Wangwe, alisema uhusiano na makubaliano yaliyopo kati ya nchi hizo, yatasaidia kubadilishana uzoefu katika shughuli zao za uzalishaji mali wanazofanya.
“Katika makubaliano haya, Watanzania wengi watapata fursa ya kuwekeza nchini Kenya, hata Kenya watawekeza nchini, hii itasaidia uchumi wa nchi yetu kukua vizuri,”alisema.
PROFESA KINYONDO
Mhadhiri wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Abel Kinyondo, alisema uhusiano wa bara moja, una faida kubwa hasa katika uzalishaji mali.
Alisema nchi za Kenya na Tanzania, zina uhusiano wa siku nyingi, hivyo makubaliano ya kimaendeleo waliojiwekea, yatasaidia kuinua uchumi wa nchi zote mbili katika suala la uzalishaji mali.
Akizungumzia kilimo, Profesa Kinyondo alisema wakati umefika, wakulima kuzalisha mazao yenye tija kwa lengo la kuyauza nchi jirani ikiwemo Kenya.
“Nina imani tuna mazao mengi ambayo yakipelekwa nchi zingine, yatazalisha mali na uchumi wetu kukua, hivyo kinachotakiwa ni kuyaongezea ubora yawe na thamani zaidi,” alisema.
Hata hivyo, Profesa Kinyondo, aliomba utiaji saini huo uwe na tija kwa nchi hizo.
“Unajua tumezoea mikataba mingi inasainiwa, lakini naomba hii isimamiwe kwa lengo la kuzalisha mali na kukuza uchumi wa nchi zote mbili.
PROFESA KWAYU
Mhadhiri wa UDSM, Dk. Emmanuel Kwayu, aliipongeza serikali kwa makubaliano waliojiwekea, ambayo yatasaidia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi kati ya nchi hizo na kuleta uhusiano mzuri.
Hata hivyo, Dk. Kwayu, alisema makubaliano hayo, yataleta fursa nyingi za kiuchumi na fedha nyingi zitaingia nchini.
“Nina matumaini makubaliano haya, nchi yetu itanufaika kwa kiasi kikubwa, kinachotakiwa ni kuongeza weledi katika shughuli tunazozifanya hasa zile za kuzalisha mali na faida tutaiona,” alisema.
Dk. Kwayu, alisema makubaliano hayo, yatakuza diplomasia ya uchumi, yatawasaidia wafanyabiashara, wakulima na sekta nyingine kufaidika nayo kwa sababu, kutakuwa na mengi yatakayozungumzwa yakiwemo yale ya kubadilishana uzoefu.
KUHUSU KUONDOLEWA VIKWAZO
Mtaalamu wa Masuala ya Uchumi kutoa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Dk. Phillip Daninga, alisema kuondolewa kwa vikwazo vya kibiashara kati ya Tanzania na Kenya, itakuwa ni hatua muhimu katika kuongeza ufanisi wa biashara kati ya nchi hizo.
Alieleza kuwa, kwa muda mrefu, vikwazo hivyo vilikuwa vikisababisha ucheleweshaji wa usafirishaji wa bidhaa na kupunguza kasi ya ukuaji biashara.
“Kwa kuwa Tanzania na Kenya ni nchi zinazotegemeana kiuchumi, kuondolewa changamoto hizo, kutasaidia kurahisisha shughuli za kibiashara na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi,” alisema Dk. Daninga.
Dk. Daninga, alisisitiza kuwa, makubaliano hayo yatafungua mazingira bora na rafiki zaidi kwa wafanyabiashara wa pande zote mbili.
“Bidhaa zitasafirishwa kwa haraka zaidi kutoka Tanzania kwenda Kenya na kutoka Kenya kuja Tanzania bila vikwazo vikubwa vya awali. Hali hii itachochea ongezeko la biashara,kuongeza ushindani wa bidhaa sokoni na kuchangia ukuaji wa uchumi wa nchi zote mbili kwa kasi zaidi,” alisema.
Kwa upande wa sekta ya kilimo, Dk. Daninga aliwataka wakulima na wafanyabiashara kutumia fursa hiyo kuongeza uzalishaji wa mazao kwa wingi zaidi.
“Kuondolewa kwa vikwazo kutarahisisha mzunguko wa bidhaa, kuongeza mapato kwa wafanyabiashara na kuharakisha ukuaji wa uchumi kwa sababu ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na Kenya ni msingi muhimu wa maendeleo endelevu kwa pande zote mbili,” alisema Dk. Daninga
Alisema kuwa uwepo wa masoko ya uhakika baina ya nchi hizo mbili ni nafasi nzuri kwa wazalishaji kupanua biashara zao na kuongeza mapato.
Pia aliwashauri kuboresha miundombinu ya usafirishaji pamoja na kuongeza mitaji kuweza kukidhi mahitaji ya soko.
Alisema makubaliano hayo yatakuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa Afrika Mashariki.
DK.RUGEIHYAMU
Mchumi na Mtaalamu wa Somo la Hisabati, Dk. Slyvester Rugeihyam alisema ujio wa Rais Ruto kuja nchini ni diplomasia iliyokomaa.
Akizungumzia suala la vikwazo kwa wafanyabiashara, Rugeihyam alisema ujio wake utaendelea kuondoa vikwazo mbalimbali vilivyokuwa vinasumbua wafanyabiashara wa pande zote mbili kushindwa kufanya shughuli zao kwa urahisi.
“Naona kuna ushirikiano mzuri kati ya wafanyabiashara wa Kenya na Tanzania kwa sababu kuna bidhaa zinauzwa zinatoka Tanzania na kuna bidhaa zinatoka Tanzania zinauzwa Kenya hilo mimi naona ushirikiano na unasababisha uchumi wetu kukua,”alisema.
JUMUIYA YA WAFANYABIASHARA
Mwenyekiti wa Jumuia ya Wafanyabiashara Nchini, Hamisi Lizembe alisema kuna ushirikiano mkubwa kati ya wafanyabiashara Kenya na Tanzania na umesababisha kuwepo mahusiano mazuri katika biashara zao.
Ushirikiano uliokuwepo umesaidia kwa kiasi kikubwa wafanyabiashara kufanya biashara pamoja huku wakishirikiana katika mahusiano ya kujenga nchi zao .
“Tunasema kuna mahusiano mazuri ni kwa sababu hivi sasa mazao ya mahindi yanayoliwa nchini Kenya yanatoka kwetu, hivyo sisi kama wafanyabiashara tunajivunia ,”alisema.
Aidha Lizembe alisema zipo bidhaa nyingi zinazouzwa nchini ambazo zimetoka Kenya.
“Wakati mwingine tunashuhudia maonesho ya wafanyabiashara Wakenya wakishiriki, naona huo ni uhusiano mkubwa uliopo.
“Hakuna vikwazo vyovyote vinavyomzuia mfanyabiashara wa kitanzania asifanye biashara yake nchini Kenya au kikwazo ambacho kinamzuia Mkenya asifanye bishara yake nchini, vingi vimeondolewa,”alisema
MIKATABA ILIYOSAINIWA
Juzi, Serikali ya Tanzania na Kenya zilisaini mikataba minane ya makubaliano yenye lengo la kuimarisha sekta mbalimbali za kimaendeleo.
Mkataba wa kwanza ulikuwa ni hati ya makubaliano kuhusu ushirikiano wa uendelezaji na usimamizi wa reli kati ya serikali ya Tanzania na Kenya, na wa pili ulihusu upembuzi yakinifu kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa bomba la gesi asilia kutoka Dar es Salaam hadi Mombasa.
Mkataba mwingine ni ulikuwa ni kuhusu usaidizi wa kisheria katika masuala ya jinai kati ya serikali hizo mbili wa nne ulikuwa ni wa makubaliano kuhusu masuala ya kilimo kati ya Tanzania na Kenya.
Mwingine ulihusu utambuzi wa vyeti vya mabaharia, wa sita ulikuwa ni hati ya makubaliano kuhusu kuimarisha ushirikiano na usimamizi wa sekta ya usafiri wa njia ya maji , mkataba wa saba ulihusu ushirikiano kati ya taasisi ya viwango Zanzibar na shirika la viwango la Kenya.
Pia wa nane ukiwa ni hati ya makubaliano kati ya vyuo vya utumishi wa umma vya Tanzania na Kenya kuhusu kujengeana uwezo katika masuala ya utumishi wa umma ambapo mikataba hiyo minane ilielezwa kuwa ishara ya ushirikiano unaozidi kuimarika kati ya Tanzania na Kenya.
Pia, nchi hizo zilikubaliana kuondoshwa kwa vikwazo visivyo vya kikodi ambapo Rais Dk. Samia aliwaagiza watendaji ifikapo Mei mwishoni viwe vimemalizika lengo ni kukuza uchumi na biashara wa Kenya na Tanzania.




