Na VICTOR MKUMBO, Morocco
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda amesema timu ya vijana wenye umri wa miaka 17 ‘Serengeti Boys’, imeiheshimisha Tanzania japokuwa haijatwaa taji la michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON U-17).
Serengeti Boys, juzi ilishika nafasi ya pili katika fainali za AFCON U 17, baada ya kufungwa mikwaju ya penalti 4-2 dhidi ya Senegal katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Moulay El Hassan, Rabat, Morocco.
Katika mchezo huo, timu hizo zililazimika kupiga penalti ili kumpata mshindi baada ya kumalizika dakika 90 kwa sare ya bao 1-1.
Akizungumza kabla ya kuondoka Rabat kurejea Tanzania, Waziri Makonda alisema vijana wa Serengeti Boys wameiheshimisha Tanzania kwa kiasi kikubwa japokuwa hawakupata nafasi ya kubeba ubingwa.
“Kila Mtanzania alitamani kuona Serengeti Boys ikiandika historia ya aina yake msimu huu katika michuano hiyo mikubwa, ilishindikana kutokana na bahati haikuwa upande wao.
“Vijana wetu wamepambana kuhakikisha wanailetea heshima Tanzania kitu ambacho wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa, kwani walipangwa na vigogo mbalimbali lakini walishinda mechi zilizopita. Hii ndiyo faida ya uwekezaji katika soka kwani vijana wamekuwa wakipata nafasi ya kusoma huku wakipewa mafunzo mbalimbali,” alisema Makonda.
Waziri Makonda alisema anamshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa ndege maalumu iliyosafirisha mashabiki na viongozi kwenda kutoa sapoti ya kutosha katika mchezo wa fainali.
Alisema kwa kiasi kikubwa vijana baada ya kuwaona mashabiki na viongozi mbalimbali walihamasika na kujituma vyema uwanjani, lakini bahati haikuwa upande wao na kuondolewa kwa mikwaju ya penalti.
Alisisitiza kwamba baada ya kumalizika kwa fainali hizo wamekutana na mawakala mbalimbali, lakini wanatarajia kukaa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), kuangalia namna ya kuwasaidia wachezaji hao.
Pia alisema baada ya michuano hiyo, safari ya Kombe la Dunia ndiyo imeanza rasmi.
Alisema kuanzia mwakani, serikali itaweka tokeni katika vituo vyote vya kukuzia vijana wenye vipaji kuhakikisha wanafikia malengo waliyojiwekea kwani ndiyo watakaoiwakilisha Tanzania katika michuano ya Kombe la Dunia mwaka 2030.
Katika michuano hiyo, Serengeti Boys ilitinga fainali kufuatia kuichapa Misri kwa mikwaju ya penalti 4-3.
KARIA AWAKALIA KOONI MAWAKALA
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia amesema wanatarajia kutengeneza utaratibu kwamba kila klabu itakayomchukua mchezaji yeyote wa Serengeti Boys, italazimika kumtumia katika mechi na siyo kumweka benchi.
Akizungumza jijini Rabat, juzi, Karia alisema kumekuwa na mawakala wa klabu mbalimbali ambao wameanza kuwawania wachezaji wa Serengeti Boys.
“Haturuhusu klabu yoyote kumchukua mchezaji na kwenda kumweka benchi kwani huo siyo utaratibu na malengo yetu,tutahakikisha wachezaji wote watakaochukuliwa na klabu tofauti, wanapata nafasi ya kucheza mechi nyingi na kuendelea kuwa na kiwango bora,”alisema.
Alifafanua kuwa mipango yao ni kuona vipaji vya wachezaji vinaendelezwa zaidi kwa mnuafaa ya nchi na siyo kuvififisha kama ilivyotokea kwa baadhi ya wachezaji.
“Tuna imani wachezaji wote watapata sehemu za kwenda kucheza.Tumeona baadhi ya mawakala wameanza kuwafuatilia wachezaji wa Serengeti Boys ambao wameonyesha kiwango bora zaidi katika michuano ya AFCON U-17,”alisema.
Hata hivyo, kiongozi huyo alisema malengo yao ni kuona vijana wanacheza zaidi mchezo wa soka na kupata nafasi katika klabu mbalimbali kuonyesha vipaji vyao.
MANARA AWATULIZA SERENGETI BOYS
Msemaji wa timu zote za Taifa za Tanzania, Haji Manara amewatuliza wachezaji wa Serengeti Boys na kuwataka kutokata tamaa japokuwa walishindwa kubeba ubingwa wa michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON U-17).
Akizungumza saa chache kabla ya kuondoka Rabat kurejea Tanzania, juzi, Manara alisema anawapongeza wachezaji wote kwa kupambana na kutinga fainali, lakini kushindwa kuchukua taji kusiwafanye wanyong’onyee.
“Vijana hamtakiwi kuonekana kama mnajisikia vibaya au kunyong’ongea baada ya kushindwa kutwaa ubingwa.Tunachotambua nyie ndiyo bora zaidi na kwamba tunaamini mtaendelea kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania kimataifa,”alisema.
Serengeti Boys ilianza michuano hiyo kwa kuifunga Msumbiji mabao 3-0, iliichapa Angola 3-0, ilipoteza mbele ya Mali kwa mabao 2-1, ikaitandika Algeria penalti 4-3 kabla ya kuirarua Misri kwa penalti 4-3.
Kwa mara ya kwanza Serengeti Boys ilishiriki michuano hiyo mwaka 2017 nchini Gabon kabla ya kucheza tena 2019 katika fainali zilizofanyika Tanzania ambapo timu hiyo ilitolewa hatua ya makundi.




