Na IRENE MWASOMOLA, Manyara
KATIBU wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kenani Kihongosi, amewaonya viongozi wa serikali na Chama wanaotunishiana misuli.
Amesisitiza kuwa, atakayefanya hivyo, atashughulikiwa katika vikao vya uamuzi.
Amesema kila mmoja aliyepewa dhamana, afahamu anamwakilisha Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, hivyo wafanye kazi kwa umoja, ushirikiano na uadilifu mkubwa.
Kihongosi alisema hayo, alipozungumza na wanachama wa Shina Namba Nane, Tawi la Tunduru, wilayani Simanjiro, mkoani Manyara.
Alisema viongozi wa Chama na serikali, wanatakiwa kufanya kazi kwa kushirikiana, hata zinapojitokeza fursa wafanye pamoja ili wananchi wafurahie maendeleo.
“Hatupaswi kutunishiana misuli au kuvimba kwa vyeo tulivyonavyo, tunachohitaji ni kazi, kama kuna mtu anaamini tunatania, afanye mambo isivyo aone, halafu tutakutana katika vikao vya uamuzi.
“Lazima kila mmoja aliyepewa dhamana afahamu anamwakilisha Rais Samia,” alisema.
Kihongosi alisisitiza kuwa, CCM haihitaji kuona vurugu wala makundi katika maeneo yoyote ikiwemo Wilaya ya Simanjiro.
Aliwataka wananchi wa Simanjiro, kuhakikisha kipaumbele chao ni usalama wao, huku akiwataka kutokubali kushawishiwa kuharibu miundombinu ya nchi kwa maslahi ya watu.
Pia, aliwataka wananchi kutokubali kupandikizwa chuki ya kuvichukia vyombo vya usalama.
“Tusipandikizwe chuki kuhusu vyombo vyetu, amani ikitoweka hutafanya jambo lolote, lazima tudumishe umoja wa kitaifa, amani na upendo wa nchi yetu,” alisema.
Kihongosi alisema CCM itabaki kuwa kimbilio la watu bila kubagua itikadi za dini, ukabila na ukanda katika kule maendeleo ya wananchi.
CAREN JOSEPH
Katibu wa Shina Namba Nane, Tawi la Tunduru, Caren Joseph, alisema eneo hilo, lina wanachama 50, kati ya hao, wanawake 23 na wanaume 27.
Alisema wanaendelea kueneza siasa na itikadi za CCM katika eneo hilo na uhai wa Chama kwa asilimia 100.




