Na AMINA KASHEBA
UONGOZI wa klabu ya Yanga umetangaza kujipanga kushirikiana na benchi la ufundi kuhakikisha timu inashinda michezo saba iliyobaki ya Ligi Kuu Tanzania Bara.
Kauli hiyo imetolewa ikiwa ni siku moja baada ya kukishuhudia kikosi chao kikifungwa mabao 3-2 na Dodoma Jiji, katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Airtel mkoani Singida.
Yanga imebakiza mechi saba kabla ya kumaliza msimu huu, katika msimamo ipo kileleni kwa pointi 54 baada ya kushuka dimbani mara 23.
Akizungumza baada ya kumalizika mchezo huo, Ofisa Habari wa klabu hiyo, Ali Kamwe alisema kila anguko lina funzo ndani yake, hivyo benchi la ufundi lina nafasi ya kujipanga na kuiongoza timu kupata ushindi katika mechi zilizobaki.
“Haikuwa siku nzuri, lakini imekuwa siku nzuri ya uongozi na benchi la ufundi kukaa chini na kufanya tathimini ya mechi saba zilizobaki, tuna kila sababu ya kujipanga na kujiweka katika nafasi nzuri ya kuiwezesha timu kutetea ubingwa wetu.”
Aliongeza “Tupo katika hatua ya mwisho ya kumalizia ligi, hivyo lazima tujipange kuhakikisha tunafikia malengo ya kutetea ubingwa,” alisema.
Alifafanua kuwa hakuna timu ambayo haijawahi kufungwa katika ligi, timu ilifanya makosa na kupoteza mchezo hivyo huu ni wakati wa kujipanga tena.
KUHUSU DJIGUI DIARRA
Akizungumzia majeruhi ya kipa namba moja Djigui Diarra, ofisa huyo alisema wanasubiri ripoti ya madaktari ili kujua aliumia kiasi gani katika mchezo dhidi ya Dodoma Jiji.
“Daktari bado hajatoa taarifa ya jeraha la kipa wetu, ripoti ikiwa tayari tutawajulisha hali yake,” alisema.
KOCHA DODOMA ATOBOA SIRI
Kocha wa Dodoma Jiji, Aman Josiah alisema siri ya wachezaji wake kupata ushindi dhidi ya Yanga ni kufuata maelekezo ambayo aliwapa baada ya kipindi cha kwanza kumalizika.
“Vijana walipokea maelekezo vizuri, kweli kipindi cha kwanza walicheza bila umakini, lakini walipambana na kufanya yale tuliyofanya, hii ni hatua nzuri kwetu,” alitamba.




