Dodoma
NA MUSSA YUSUPH
HATUA zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kuongeza ushirikiano wa kidiplomasia na mataifa mbalimbali, zimewezesha kufungua fursa za kibiashara nje ya nchi kupitia sekta ya mifugo na uvuvi.
Takwimu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, zimebainisha hadi kufikia Aprili mwaka huu, tani za nyama 12,763.77 zenye thamani ya dola 54,654,931.61 (zaidi ya sh. bilioni 142) zimeuzwa katika masoko ya nchi mbalimbali, ikilinganishwa na tani 9,913.61 zenye thamani ya dola 40,366,846.3 (zaidi ya sh. bilioni 104) zilizouzwa kipindi kama hicho katika mwaka wa fedha wa 2024/2025 sawa na ongezeko la asilimia 22.3.
Kiasi hicho kinajumuisha tani 8,228.48 za nyama ya mbuzi, tani 3,787.38 nyama ya kondoo, tani 675.31 nyama ya ng’ombe, tani 38.60 nyama ya nguruwe na tani 33.90 nyama ya kuku.
Akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini hapa jana, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Dk. Bashiru Ally, alisema katika kipindi hicho, nyama kutoka Tanzania ziliuzwa katika masoko ya nchi za Bahrain, Comoro, Hong Kong, Kenya, Kuwait, Oman, Qatar, Saudi Arabia, Ushelisheli, Umoja wa Falme za Kiarabu na Vietnam.
BIASHARA YA NGOZI
Kwa upande wa biashara ya ngozi, alisema biashara hiyo imeendelea kuimarika na kuchangia katika Pato la Taifa.
Alisema hadi kufikia Aprili mwaka huu, vipande vya ngozi ghafi 2,273,160 vyenye uzito wa kilo 7,081,784 (ng’ombe vipande 1,107,533 mbuzi vipande 815,939 na kondoo vipande 349,688) vyenye thamani ya sh. bilioni nane viliuzwa.
Dk. Bashiru alisema vipande hivyo vya ngozi viliuzwa katika nchi za Nigeria, Kenya, Djibouti, Ethiopia, China, Ghana, Togo na Pakistan, ikilinganishwa na vipande vya ngozi 1,651,088 vyenye uzito wa kilo 6,287,881 (ng’ombe vipande 1,232,833, mbuzi vipande 298,978 na kondoo vipande 119,277) vyenye thamani ya sh. bilioni 7.95 vilivyouzwa Nigeria, Kenya, Djibouti, Ethiopia, China na Pakistan mwaka 2024/2025.
“Mauzo ya ngozi kwenda nje ya nchi yameongezeka kutokana na mahitaji ya soko la ngozi isiyosindikwa kuongezeka katika nchi za Nigeria, Kenya na Togo.
“Pia, wizara imewawezesha wamiliki wa machinjio ya kisasa yaliyopo chini ya Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Huru Maalumu ya Kiuchumi (TISEZA) kwa kuwaondolea kodi ya kusafirisha ngozi nje ya nchi.
Alisisitiza: “Hatua hii imeleta mafaniko ya kupata soko la ngozi za mbuzi na kondoo kusafirishwa kwa kiwango kikubwa kwenda nchini Kenya kwa kuwa hadi kufikia Aprili mwaka huu, tani 12,763.77 zenye thamani ya dola 54,654,931.61 ziliuzwa katika masoko ya nchi mbalimbali, sawa na ongezeko la asilimia 22.3,” alisema.
Alibainisha kiasi hicho kinajumuisha tani 8,228.48 za nyama ya mbuzi, tani 3,787.38 za nyama ya kondoo, tani 675.31 za nyama ya ng’ombe, tani 38.60 za nyama ya nguruwe na tani 33.90 za nyama ya kuku.
MAUZO YA VIFARANGA YAPAA
Kwa mujibu wa Dk. Bashiru, mauzo ya vifaranga kwenda nje ya nchi yameongezeka kutoka vifaranga 1,909,078 mwaka 2024/2025 hadi vifaranga 5,751,584 mwaka 2025/2026.
Alisema ongezeko la mauzo ya vifaranga nje ya nchi limechangiwa na kuimarika kwa uzalishaji, udhibiti magonjwa na uanzishwaji mashamba makubwa yanayofuga kuku kibiashara.
MAZAO YA UVUVI YAONGEZEKA
Waziri huyo alisema katika mwaka 2025/2026, biashara ya mazao ya uvuvi katika soko la ndani imeendelea kuimarika ambapo hadi Aprili mwaka huu, tani 439,673.63 zenye thamani ya sh. bilioni 4.1 ziliuzwa katika soko la ndani ikilinganishwa na tani 422,639.10 zenye thamani ya sh. bilioni 2.8 zilizouzwa mwaka 2024/2025.
Alisema kuimarika biashara ya samaki katika soko la ndani kumetokana na kuimarika miundombinu ya ubaridi kuhifadhi mazao ya uvuvi na miundombinu ya usafirishaji mazao ya uvuvi.
TANZANIA KINARA UZALISHAJI MWANI
Katika hotuba yake, Dk. Bashiru alisema Tanzania imeendelea kuwa kinara wa uzalishaji mwani Afrika ambapo hadi Aprili mwaka huu, tani 132,479.29 za mwani zenye thamani ya sh. bilioni 13.9 zimezalishwa ikilinganishwa na tani 88,615.2 zenye thamani ya sh. bilioni 9.3 zilizozalishwa katika mwaka 2024/2025, sawa na ongezeko la asilimia 49.5.
“Ongezeko hilo linatokana na hatua za serikali kuhamasisha uzalishaji kwa kuwapatia wakulima wa mwani mafunzo, pembejeo, kuhamasisha matumizi ya bidhaa zitokanazo na mwani pamoja na kuimarika kwa soko,” alisisitiza.
BOTI YA UVUVI
Katika kuimarisha Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) alisema wizara kupitia ufadhili wa Programu ya Kuendeleza Uchumi na Jamii (SDP) ya Japan, imekamilisha ununuzi wa meli ya kisasa (TAFICO FV.01) kwa ajili ya uvuvi wa Bahari Kuu yenye urefu wa meta 22 ambayo ilizinduliwa rasmi Aprili mwaka huu na Rais Dk. Samia.
Alisema meli ya aina hiyo ni ya kwanza kumilikiwa na serikali kupitia TAFICO ambayo itaendesha shughuli za uvuvi wa
bahari kuu kwa utaratibu wa ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP).
“Upatikanaji meli hii ni hatua ya kimkakati katika kuimarisha shirika la TAFICO na kutumia fursa za uchumi wa buluu katika kufanya mageuzi kwenda uvuvi wa kisasa na uzalishaji wenye tija kuliwezesha shirika kujiendesha kibiashara na kuongeza mchango wa sekta ya uvuvi katika pato la Taifa,” alisisitiza.
CHANJO YA MIFUGO
Waziri huyo alisema serikali imeendelea kuratibu utekelezaji kampeni ya chanjo na utambuzi mifugo kitaifa ambapo hadi kufikia Aprili mwaka huu, ng’ombe 9,115,297 sawa na asilimia 47.37 ya lengo wamechanjwa dhidi ya Homa ya Mapafu ya Ng’ombe (CBPP).
Pia, alisema mbuzi na kondoo 2,672,237 sawa na asilimia 15.51 wamechanjwa dhidi ya ugonjwa wa Sotoka (PPR) na kuku 38,833,603 sawa na asilimia 97.08 wamechanjwa dhidi ya Mdondo, Ndui na Mafua ya Ndege.
Kadhalika, alisema jumla ya mifugo 2,566,887 imewekewa hereni za kielektroniki kwa ajili ya utambuzi
MKAKATI KUDHIBITI MIGOGORO YA WAKULIMA NA WAFUGAJI
Dk. Bashiru alisema wizara imeendelea kuimarisha mikakati ya udhibiti migogoro baina ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi kwa kushirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Alisema katika mwaka 2025/2026, serikali imewatambua wafugaji 3,021 katika halmashauri za Mvomero, Gairo, Kilombero, Kilosa, Malinyi, Ulanga, Mlele, Sikonge, Kaliua, Urambo, Bahi, Kibaha, Mbarali, Magu na Sengerema.
“Hatua hizo zinalenga kuwapatia wafugaji elimu ya umiliki wa ardhi, matumizi endelevu ya rasilimali za malisho na
kuhamasisha upangaji matumizi bora ya ardhi ili kulinda maslahi ya watumiaji wengine wa ardhi,” alisisitiza.
MAONI YA KAMATI
Akiwasilisha maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mjumbe wa kamati hiyo, Keneth Nollo, alisema kukosekana viwanda vya uhakika vya mazao ya mifugo na uvuvi nchini ikiwemo maziwa, ngozi,
kwato, pembe na mazao ya baharini kunaathiri mchango wa Sekta ya Uvuvi na Mifugo katika uchumi.
Pia, alisema vikwazo vinavyosababisha mazao ya mifugo na uvuvi yanayozalishwa nchini kukosa masoko nje ya nchi ikiwemo ubora wa bidhaa, vinahitaji kufanyiwa kazi.
“Serikali itoe elimu kwa wavuvi kuhusu madhara ya uvuvi haramu ambao unaathiri mazalia ya samaki na kuchangia
uhaba wa samaki nchini. Serikali isimamie uvuvi endelevu na uzingatiaji sheria zinazosimamia shughuli zote za uvuvi na uhifadhi wa mazingira.
Alisisitiza: “Serikali ikamilishe ununuzi meli mbili zitakazowezesha kuvua eneo la Bahari Kuu kama ilivyoelekezwa na ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2025. Hatua hii itaongeza upatikanaji wa mazao yatokanayo na uvuvi kwa ajili ya matumizi ya ndani na kuongeza mauzo nje ya nchi.”
Ili kutekeleza vipaumbele mbalimbali katika mwaka wa fedha 2026/2027, Dk. Bashiru aliliomba Bunge kuiidhinishia wizara hiyo sh. bilioni 433.3.
Alisema kati ya fedha hizo, sh. bilioni 98.2 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida huku sh. bilioni 335 ni kwa ajili ya miradi yamaendeleo.




