Musoma
Na IRENE MWASOMOLA
KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kenani Kihongosi, amesema hakuna mkubwa kuliko Chama.
Amesema endapo Chama kikibaini kuna mtu anataka kukiharibu, kitamshughulikia bila kujali umaarufu wala cheo alichonacho.
Aidha, amesisitiza kuwa CCM itaendelea kulinda hadhi yake, hivyo asitokee mtu akajiona mkubwa kuliko Chama na kwamba kina misingi imara inayoendelea kusimamiwa tangu kilipoasisiwa.
Kihongosi alieleza hayo alipokuwa akizungumza na wanachama wa Shina Namba Tano, Kata ya Mwisenga, mjini Musoma mkoani Mara, ambapo aliwataka viongozi kuanzia ngazi ya shina kuendelea kuweka maslahi ya Chama mbele na siyo ya mtu binafsi.
Alisema CCM ni taasisi siyo mali ya mtu, hivyo vyama vingine vijifunze kwa sababu vipo ambavyo kiongozi mmoja akiondoka navyo vinakufa.
“Asije akatokea mtu akajiona yeye ni mkubwa kuliko Chama, anajidanganya kwa kuwa Chama hiki kina misingi na utaratibu tangu kilipoasisiwa.
“Chama hakijawahi kukosea hata siku moja, uamuzi wa Chama lazima uheshimiwe na watu wote, hakuna mkubwa kuliko CCM na ukitaka kuamini hilo wewe ondoka katika uongozi wa Chama kuwa raia wa kawaida uone kama utakuwa na heshima, heshima yako ni kwa sababu ya Chama Cha Mapinduzi,” alisema.
Pia, alisema Chama kikijua mtu anataka kuharibu kitamshughulikia bila kujali umaarufu na cheo alichonacho.
Vilevile, Kihongosi aliwataka viongozi wa CCM ngazi zote kulinda heshima na hadhi ya Chama kwa mienendo mbele ya wanaowaongoza.
Alisema CCM itabaki kuwa Chama kiongozi mkoani Mara na taifa kwa ujumla.
Kwa mujibu wa Kihongosi, amekwenda mkoani Mara kuona fedha zinazotolewa na serikali zimefanya kazi gani na kwamba hiyo ndiyo kazi ya Chama.
Pia, aliwataka wana CCM kuendelea kushiriki vikao vya mashina, kuishi kwa upendo, umoja na mshikamano.
“Vikao vya Chama viwe ajenda endelevu, tuendelee kuvifanya, pia wana CCM na Watanzania wote tuendelee kuishi kwa umoja na mshikamano,” alisisitiza.
Awali, Katibu wa Shina Namba Tano, Kata ya Mwisenga, Emiliana Kuboja, alisema shina hilo lina wanachama 50 na kati yao 35 wameshalipa ada ya uanachama.
Emiliana alisema shina hilo linajivunia mafanikio mbalimbali ikiweko kushinda uchaguzi kwa kishindo nafasi zote ukiwemo ubunge, udiwani na urais.
Daud Magabe mkazi wa eneo hilo, alisema wanakabiliwa na kero ya ubovu wa barabara ikiwemo inayokwenda katika Shule ya Msingi Mwisenga, aliyosoma Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere.
Alisema mwaka 2019 serikali iliahidi kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami, lakini ahadi hiyo bado haijatimia.
Kihongosi yupo mkoani Mara kwa ziara ya siku nne ambayo ilianza jana na inatarajiwa kuhitimishwa Mei 17, mwaka huu.
Ziara hiyo imelenga kukagua utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM, kuangalia uhai wa Chama kuanzia ngazi ya shina na kutembelea miradi ya maendeleo.



