Na MWANDISHI WETU
RAIS wa Shirikisho la Chama cha Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Tumaini Nyamhokya amewataka wanahabari kuwahamasisha waajiri nchini kuhusu umuhimu wa kuripoti kwa wakati matukio ya ajali, ugonjwa ama vifo vinavyotokana na kazi, katika Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), kurahisisha utolewaji wa fidia kwa wakati.
Nyamhokya ameyasema hayo jijini Dar es Salaam leo ,akifungua mafunzo kuhusu Fidia kwa Wafanyakazi kwa Wanachama wa Chama cha Waandishi wanaofanya kazi katika vyombo vya Habari (JOWUTA).
Amesema lengo la kuanzishwa kwa mfuko huo ni kushughulikia masuala ya fidia kwa Wafanyakazi waliopo katika sekta ya umma na binafsi Tanzania Bara ambao wataumia, kuugua ama kufariki kutokana na kazi wanazozifanya kwa mujibu wa mikataba ya ajira zao.
Vilevile, amesema WCF inatoa mafao mbalimbali ikiwa ni pamoja na huduma za matibabu, fidia ya ulemavu wa muda na wakudumu, malipo kwa anayemhudumia mgonjwa, malipo kwa wategemezi endapo mfanyakazi atafariki, huduma za utengemao, na msaada wa mazishi.
” Mafao haya yanatolewa kwa wafanyakazi au wategemezi wa wafanyakazi watakaopata ajali, ugonjwa au kifo kutokana na kazi zao. Ndio maana ninawaambia kuwa WCF ni taasisi yetu na hivyo tuna wajibu kuhakikisha tunaulinda kwa nguvu zote kuhakikisha unakuwa himilivu.”amesema Nyamhokya .
Aidha,Nyamhokya amewataka waandishi wa habari kuwaelimisha wafanyakazi juu ya umuhimu wa kujiunga na vyama vya wafanyakazi kwa ajili ya kuunganisha nguvu katika kutetea maslahi yao.
“Slogan yetu ya ‘SOLIDARITY FOREVER’ inamaanisha umuhimu wa umoja na mshikamano katika kutetea maslahi ya wafanyakazi. Wafanyakazi ni jeshi kubwa lakini bila kuwa wamoja hatuwezi kufanikiwa katika mapambano ya kudai haki zetu” amesema.




