Na MWANDISHI MAALUMU-Mwanza
MKOA wa Mwanza umetajwa kuwa kinara kwa kuratibu na kusimamia ipasavyo shughuli za kukabiliana na maafa, majanga na mawasiliano ya dharura kutokana na hatua za kuimarisha mifumo ya utayari na mwitikio wa dharura.
Sifa hizo zimetolewa Juni 4, 2026 na wataalamu wa Ofisi ya Waziri Mkuu wakati wa mafunzo ya Kamati za Usimamizi wa Maafa yanayofanyika mkoani Mwanza kwa siku mbili yakilenga kuongeza uwezo wa kukabiliana na majanga.
Akifungua mafunzo hayo, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda amesema maafa yameendelea kuwa tishio kubwa duniani kutokana na athari zake kwa maisha ya watu, uchumi na maendeleo ya jamii.
Ametaja baadhi ya majanga yanayoikabili Tanzania ni mafuriko, ukame, maporomoko ya ardhi, matetemeko ya ardhi, mioto ya misitu na magonjwa ya mlipuko.
Kutokana na kuongezeka matukio, Mtanda amezitaka wilaya zote mkoani Mwanza kuwa na mipango kazi na mifumo imara ya usimamizi wa maafa katika kuhakikisha maandalizi, mwitikio wa haraka na urejeshaji hali unafanyika kiufanisi.
Ameongeza serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuimarisha usimamizi wa maafa kwa kutumia Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa ya mwaka 2024 pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya mwaka 2022.
Mkuu wa Mkoa ameeleza mafunzo hayo yatawajengea uwezo viongozi na wataalamu katika utekelezaji wa sera, sheria na miongozo ya usimamizi wa maafa katika maeneo yao.
Aidha, ameipongeza serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kusaidia waathirika wa mafuriko wilayani Kwimba tani tisa za mahindi, mablanketi, ndoo na vifaa vya wanafunzi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa eneo la utafiti kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bw. Vanvaco Luvanda amesema mafunzo hayo ya siku mbili yanaendelea kutolewa nchini kote kwa lengo la kuongeza utayari na uwezo wa kitaalamu wa kukabiliana na maafa yanapotokea.
Amefafanua mafunzo hayo yamekuja kwa wakati muafaka, ambapo uzoefu unaonesha athari za maafa zinaendelea kuongezeka kutokana na mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la shughuli za kibinadamu na changamoto nyingine zinazoweza kusababisha maafa.



