Na NASRA KITANA
LEO siku ya kilio au kicheko, kwa timu za Yanga na Simba zitakaposhuka kucheza viwanja tofauti katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Timu hizo zitashuka dimbani katika michezo ya ligi hiyo kuwania ubingwa ambapo timu zote 15 zinazoshiriki michuano hiyo, zitacheza katika viwanja tofauti.
Yanga na Simba watakuwa nyumbani katika mechi zake za ligi, huku kila mmoja akimuombea mwenzake apote.
Hali hiyo, inakuja huku Yanga ikiwa inaongoza ligi hiyo kwa ponti 69, wakati Simba yenyewe ina pointi 67 huku Azam FC ikishika nafasi ya tatu, ina alama 58.
Pamoja na vita ya Yanga na Simba, bado kuna timu zinaendelea kupambana kukwepa kushuka daraja huku KMC tayari imeshuka.
Mabingwa watetezi wa kombe hilo, Yanga watashuka dimbani kupambana na TRA United katika mchezo utakaopigwa Uwanja wa KMC.
Akizungumza jana, Kocha Mkuu wa Yanga, Abdihamid Moalin alisema kikosi chake kimejipanga kushinda katika mchezo huo.
“Tunaingia katika mchezo huo kwa kuwaheshimu wapinzani wetu, tutapambana kupata ushindi na kuendelea kuongoza ligi,” alisema Moalin.
Nyota wa timu hiyo, Abuutwalib Mshery alisema mechi hiyo ni muhimu zaidi kwao ili kupata matokeo mazuri.
Kocha wa TRA United, Etienne Ndairagije alisema wamefanya maandalizi ya kutosha kuhakikisha wanapata ushindi leo.
“Yanga siyo timu ya kuibeza, tunahitaji kupambana nao mwanzo mwisho ili kupata ushindi katika mchezo huo muhimu, tutapambana kwa nguvu zote,” alisema Ndairagije.
Naye nyota wa TRA United, Shaban Chilunda alisema wamejipanga vizuri na wachezaji wote wana hamu ya kucheza mchezo huo.
Kwa upande wa Simba, itacheza leo na timu ya Singida Black Stars katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, kocha wa Simba Steve Barker alisema timu yao imejipanga vizuri kuhakikisha wanapata ushindi katika mchezo wa leo.
“Huu ni mchezo mgumu na wenye changamoto kubwa kwani Singida ni timu bora na yenye wachezaji bora hivyo tutapambana mwanzo mwisho kupata ushindi katika mchezo huo muhimu,” alisema.
Barker alisema wanachokihitaji katika mchezo huo ni kuhakikisha wanatumia vizuri nafasi watakazozipata na kuibuka na ushindi.
Mchezaji wa Simba, Antony Mligo alisema zinapokutana timu hizo mbili haiwezi kuwa mechi nyepesi.
Kocha Mkuu wa Singida Black Star, Muhibu Kanu alisema amekiandaa vizuri kikosi chake kiweze kupambana kupata ushindi.
“Tunaenda kutumia kaosoro za Simba, tupate matokeo mazuri, tayari tushakata tiketi ya kucheza michuano ya kimataifa, hivyo mechi zilizobaki ni za kusherekea mafanikio yetu,” alisema Kanu.
Mechi nyingine ni Azam Fc dhidi ya Coastal Union, Namungo Fc na Fountain Gate FC, Pamba Jiji na JKT Tanzania, Mashujaa FC kupambana na KMC, Tanzania Prisons ikimenyana na Mtibwa Sugar huku Dodoma Jiji ikipambana na Mbeya City.
Mechi zote hizo zitachezwa saa 10:00 jioni katika viwanja tofauti.



