Na Suleiman Jongo, Beijing – China
CHINA imezihakikishia nchi za Afrika kuwa, itaendeleza ushirikiano wenye manufaa kwa lengo la kufanisha jitihada za kujiendeleza kichumi na kupiga hatua kubwa za maendeleo.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya China, Shuai Guipeng, alipokuwa akizungumza kuhusu Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) na Sera ya Kuondoa Ushuru wa Forodha kwa Bidhaa za Afrika zinazoingizwa nchini humo, alipokutana na wahariri wa vyombo vya habari kutoka Afrika, jijini Beijing.
Wahariri hao wanahudhuria mkutano wa vyombo vikuu vya habari vya Afrika, ulioandaliwa na China ukiwa na mada mbalimbali kuhusu hatua za maendeleo zilizofikiwa na nchi hiyo na sera zake kuhusu ushirikiano na nchi zingine.
Shuai alisema nchi za Afrika zina nafasi kubwa ya kufikia ya kujiendeleza kutokana na uwepo wa rasilimali mbalimbali na kwamba serikali ya China itaendelea kushirikiana nazo kufanikisha hatua hiyo.
Alisema China imeendelea kuchukua hatua ikiwamo kuanzisha majukwaa ya ushirikiano kama FOCAS ambalo lengo lake ni kuzikutanisha nchi hizo kukaa pamoja kujadili changamo na fursa zilizopo kujiendeleza.
“China imeendelea kuwa mshirika wa kweli, wa karibu kwa nchi za Afrika kwa lengo la kusaidia kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kuimarisha ushirikiano wa watu.
“Tumeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwamo kuanzisha FOCAC jambo ambalo limeigwa na wengine. Tunavisihi vyombo vya habari kuwa daraja la kutambua na kufungua fursa zilizopo kwa maendeleo ya pande zote,” alisema.
Akitaja hatua nyingine zinazoendelea kuchukuliwa kuimarisha ushirikiano wa Afrika na China na kufungua milango ya maendeleo, alisema uamuzi wa kuziondolea ushuru wa forodha bidhaa za Afrika zinazoingizwa katika soko la China umeanza kuzaa mafunda kwa baadhi ya nchi kuongeza uwezo wake wa kuuza bidhaa za kilimo nchini humo.
Kwa mujibu wa Shuai, miongoni mwa nchi za mfano zilizotumia vizuri fursa hiyo ni Tanzania ambayo imeongeza mauzo yake baadhi ya bidhaa hususan za kilimo katika soko hilo.
Wakizungumzia ushirikiano wa China na Afrika baada ya kukutana na mkurugenzi huyo, baadhi ya wahariri walisema China ni rafiki wa kweli anayestahili kukumbatiwa kwa kuwa amekuwa bega kwa bega katika safari ya maendeleo ya nchi za Afrika.
“China ni rafiki wa kweli, anastahili kuwekwa karibu zaidi kwa maendeleo ya Afrika kupitia ushirikiano katika utatuzi wa changamoto na kufungua fursa,” alisema Angela Chishimba, Mhariri kutoka gazeti la Zambia Daily Mail la Zambia. Kwa upande wake Ezekiel Mwambopo kutoka kituo cha Televisheni cha Channel 10, Tanzania alisema alama za wazi zinazowekwa na China katika maendeleo ya Afrika ukiwemo mchango wake katika ujenzi wa miundombinu muhimu kama reli ya TAZARA, ni kielelezo tosha cha nia njema ya nchi hiyo kuona Afrika inainuka kiuchumi.




