Na ATHNATH MKIRAMWENI
WAZIRI Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba amewatangazia vita wakandarasi wote wanaotumia vibaya fedha za miradi ya umma na kushindwa kuwalipa wafanyakazi, akisema serikali haitavumilia uzembe unaowaumiza wananchi.
Dk. Mwigulu alitoa kauli hiyo alipokuwa akipokea taarifa ya ujenzi wa barabara ya Mbauda-Losinyai na T/Packers yenye urefu wa kilomita 70.
Akisikiliza na kutatua kero za wananchi, Mwigulu alibaini kuwa baadhi ya wakandarasi hulipwa fedha zote na serikali, lakini wanakwepa kulipa vibarua hivyo kusababisha miradi ichelewe kukamilika kwa wakati.
Dk. Nchemba alisema kitendo hicho ni uhujumu wa wazi kwa wananchi waliolipa kodi zao kwa matarajio ya kuona maendeleo yakitekelezwa kwa wakati na kwa ubora unaostahili.
“Serikali inalipa fedha kwa ajili ya miradi, lakini haiwezekani mkandarasi anachukua fedha halafu anashindwa kuwalipa waliotekeleza kazi. Hili halikubaliki,” alisisitiza.
Alionya kuwa, wakandarasi wote watakaobainika kufanya udanganyifu au uzembe watachukuliwa hatua kali, ikiwemo kunyimwa kabisa fursa ya kupewa miradi mingine ya serikali.
Katika hatua nyingine, alisema serikali imeanzisha mfumo mpya wa kufuatilia utekelezaji wa miradi na kero za wananchi, ambapo kila mwisho wa mwezi taarifa za mikoa zitawasilishwa kwa tathmini.
Dk. Nchema alisema viongozi wataanza kuwasiliana moja kwa moja na wananchi waliowasilisha malalamiko kuthibitisha kama changamoto zao zimepatiwa ufumbuzi.
“Baada ya kusikiliza kero za wananchi, napata jedwali la kila mwisho wa mwezi, likionyesha matatizo yaliyowasilishwa na hatua zilizochukuliwa. Sitabaki na karatasi tu, nampigia mwananchi mmoja mmoja kuthibitisha kama kweli kero yake imetatuliwa, sasa asiyetekeleza atachukuliwa hatua,” alisema.
Mbali na suala la wakandarasi, wananchi walipata nafasi ya kueleza kero mbalimbali ikiwemo migogoro ya ardhi, kudhulumiwa mali, ucheleweshaji wa haki zao pamoja na changamoto za biashara.
Baadhi ya wananchi walieleza masikitiko yao kutokana na kucheleweshwa kwa haki kwa muda mrefu licha ya kufuata utaratibu wa kisheria ambapo Waziri Mkuu alisisitiza kuwa, hakuna mwananchi atakayenyimwa haki yake endapo ushahidi utakuwepo, akiahidi kusimamia kwa karibu kila suala lililowasilishwa.
ONYO KWA WATENDAJI KUZOEA MALALAMIKO
Pia, Dk. Nchemba aliwakumbusha na kusisitiza watendaji wa serikali kuacha tabia ya kuzoea malalamiko ya wananchi bila kuyatatua, akisema kuwa sasa ni wakati wa kuwajibika ipasavyo.
“Hatutaki kusikia kero zinazojirudia bila suluhisho. Kila tatizo lina majibu na lazima lipatiwe ufumbuzi,” alisema.
Dk. Nchemba alisema serikali ipo kwa ajili ya wananchi na itaendelea kuhakikisha kila mmoja anapata huduma stahiki bila upendeleo.
Vilevile, alisisitiza umuhimu wa amani na kuwataka wananchi kuepuka vitendo vinavyoweza kuvuruga utulivu wa nchi kwa sababu maendeleo hayawezi kupatikana bila mazingira ya amani.
Aliwahakikishia wananchi kuwa, serikali iko macho na itaendelea kuchukua hatua dhidi ya wanaokwamisha maendeleo, huku akitoa wito kuendelea kutoa taarifa za changamoto zao bila woga.
KUHUSU FIDIA
Waziri Mkuu alisisitiza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan aliagiza wananchi wasinyang’anywe maeneo yao bila kupewa fidia.
“Kama kutakuwa na maeneo yanahitajika kwa ajili ya miradi ya kimkakati au maslahi mapana itahakikisha kila aliye mmiliki halali wa eneo husika anapata haki yake.
“Mimi nielekeze watu wasije wakaondolewa bila utaratibu kufuatwa ili yeyote ambaye manufaa mema yanamfuata katika eneo lake naye aweze kubadilisha maisha yake,” alisema.
Waziri wa Ujenzi, Abdalla Ulega alisema wamepokea sh. bilioni 10.2 za kuwalipa fidia wananchi 52 waliopisha ujenzi wa mradi huo wa barabara.
Kwa upande wake, Waziri Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, ambaye ni Mbunge wa Arusha Mjini, Paul Makonda alimshukuru Rais Dk. Samia kwa maendeleo na miradi mikubwa inayotekelezwa mkoani humo.
Katika hatua nyingine waziri mkuu aliwaagiza wakandarasi wanaojenga barabara za kuelekea Uwanja wa Samia Stadium utakaotumika kwa michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027 kufanya kazi usiku na mchana.
Pia, waongeze nguvu kazi na vitendea kazi ili wakaguzi wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF) watakapokuja kufanya ukaguzi kusiwe na dosari zozote.
Aidha amemshukuru Rais Dk. Samia kwa kuridhia Tanzania kuwa moja ya nchi wenyeji wa mashindano hayo.




