Na FRED ALFRED, Dodoma
SERIKALI imepanga kutoa vibali vya ajira 45,000 za kada mbalimbali kujaza nafasi katika taasisi za umma kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Hayo yalibainishwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, alipokuwa akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka huo wa fedha.
“Katika mwaka 2026/2027, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma imepanga kushughulikia vibali vya nafasi 45,000 za ajira mpya kwa ajili ya kujaza nafasi zitakazoidhinishwa katika ikama za taasisi za umma na kuzihakiki,” alisema.
Pia imepanga kuidhinisha madai ya malimbikizo ya mishahara ya watumishi wa umma katika taasisi 425.
YAOMBA SH. TRILIONI 1.5
Kwa mujibu wa Kikwete, ofisi hiyo imeliomba Bunge kuidhinisha matumizi ya jumla ya sh. trilioni 1.5 katika mwaka wa fedha 2026/2027.
Alisema kati ya fedha hizo, sh. trilioni 1.4 zimetengwa kwa matumizi ya kawaida, huku sh. bilioni 163 zikielekezwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Katika hatua nyingine, Kikwete alisema hadi Machi mwaka huu, jumla ya wasailiwa 91,126 katika ajira za serikali walipangiwa vituo vya kazi, huku ujazaji wa nafasi 12,722 ukiendelea.
Alisema wasailiwa 41,102 wamehifadhiwa katika kanzidata baada ya kufaulu usaili wa mahojiano, wakiwemo wanaume 21,899 na wanawake 19,203 wa kada mbalimbali.
Vilevile, alisema katika kipindi hicho, saili sita za mchujo zilifanyika kutokana na waombaji ajira 845,042 kuwasilisha maombi, ambapo wanaume walikuwa 490,514 na wanawake 354,528.
“Jumla ya wasailiwa 9,836 walifanya usaili wa vitendo, wakiwemo wanaume 6,928 na wanawake 2,908. Ujenzi wa mfumo wa kupima haiba na tabia kwa wasailiwa umekamilika na kwa sasa upo katika hatua za majaribio,” alisema.
AJIRA 43,866
Ridhiwani alisema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi mwaka huu, ofisi hiyo pamoja na taasisi zake imeboresha utendaji kazi serikalini kwa kuimarisha upatikanaji na usimamizi wa rasilimali watu kwa kutoa vibali vya ajira 43,866 katika sekta mbalimbali.
Alisema serikali imeidhinisha ajira mbadala, uhamisho, likizo bila malipo na nafasi za uongozi zaidi ya 7,000, hatua iliyoongeza ufanisi wa kiutendaji na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
“Serikali imehakiki na kulipa madai ya mishahara na malimbikizo kwa zaidi ya watumishi 14,600 yenye thamani ya zaidi ya sh. bilioni 22, hatua iliyoongeza motisha na ufanisi kazini kwa watumishi wa umma. Uboreshaji wa mifumo ya kiutumishi umeimarisha usimamizi wa rasilimali watu na kuongeza tija katika utoaji huduma za serikali,” alisema.
MATAMKO YA VIONGOZI
Akizungumzia matamko ya viongozi, alisema serikali kupitia Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma imeimarisha maadili ya viongozi wa umma, ambapo asilimia 85 ya viongozi wamewasilisha matamko ya mali na madeni.
Alisema hatua hiyo inaonesha kuimarika kwa uwajibikaji wa viongozi na kuongeza uaminifu wa wananchi kwa taasisi za umma ikiwa sehemu ya juhudi za kujenga serikali inayowajibika, yenye uwazi na inayoaminika.
“Wananchi 34,334 wamepatiwa elimu ya maadili, hatua ambayo inachangia kukuza utamaduni wa uadilifu na uwajibikaji katika jamii. Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kusimamia maadili kwa vitendo kwa sababu uadilifu wa viongozi ndio msingi wa haki, maendeleo na imani ya wananchi kwa serikali yao,” alisema.
Aliongeza kuwa serikali itaendelea kuwekeza katika kuwajengea uwezo watumishi wake, kwa kuwa mtumishi bora ni msingi wa huduma bora kwa mwananchi.
Jumla ya viongozi 4,867 walitia saini hati ya ahadi ya uadilifu, ambapo wanaume ni asilimia 69 na wanawake asilimia 31.
KUUNGANISHA MIFUMO YA SERIKALI
Kwa mujibu wa Ridhiwani, serikali imeboresha utoaji huduma kwa wananchi kwa kuwekeza katika mfumo wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).
Alisema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, jumla ya mifumo 252 ya serikali imeunganishwa katika mtandao, hatua ambayo inawawezesha wananchi kupata huduma kwa urahisi, haraka na bila ulazima wa kufika ofisini, hivyo kupunguza gharama na muda.
“Uboreshaji huo umepunguza urasimu katika utoaji wa huduma na kuongeza uwazi, na hatimaye kuimarisha uwajibikaji katika taasisi za umma,” alisema.



