Na MUSSA YUSUPH,
Arusha
MAKAMU Mwenyekiti Mstaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Abdulrahman Kinana, ameyataja mambo matatu ambayo Mgombea Urais kupitia CCM, Dk. Samia Suluhu Hassan ameyatekeleza kwa ujasiri mkubwa na kuthibitisha uwezo wake katika kuendelea kuliongoza Taifa.
Ameyataja mambo hayo ni utekelezaji wa ilani ya CCM, ahadi za aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dk. John Magufuli na ahadi ambazo Dk. Samia, alizitoa katika ziara zake mbalimbali kwa wananchi.
Akizungumza katika mkutano wa kampeni uliofanyika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha, Kinana amesema Dk. Samia, ametekeza kwa vitendo mambo hayo matatu kwa ujasiri mkubwa.
“Ilani ya CCM imetekelezwa, ahadi za mgombea zimetimizwa kwa asilimia 100, ahadi zake binafsi alizozitoa alipotembelea wananchi mikoani, nazo amezitekeleza kwa asilimia 100.
“Taifa linahitaji kiongozi mwenye busara, ushirikiano wa dhati na wenzake ili kuongoza kwa kuweka vipaumbele vinavyotekelezeka ambapo Dk. Samia amethibitisha sifa hizo,”amesema.
Kinana ameeleza kuwa, kazi za Dk. Samia, zimeonekana kila kata na kila mkoa nchini, huku mashahidi wa kweli ni wananchi wanaofaidika kupitia miradi mbalimbali.
Pia, amesema kauli mbiu ya CCM katika uchaguzi mkuu ya ‘Kazi na Utu’ ina maana kubwa, kwani inatambua msingi wa utu na haki kwa Taifa.
“Baba wa Taifa alikuja na kauli mbiu Uhuru na Kazi, baadaye ikaja Uhuru ni Kazi, leo tunasema Kazi na Utu. Dk. Samia ameonyesha mfano bora, anafanya kazi kwa kujituma na kuwajali Watanzania wote,” alisema.
Ametoa wito kwa Watanzania kujitokeza kwa wingi ifikapo Oktoba 29, mwaka huu kumpa kura Dk. Samia kwa kuwa, ameonesha uongozi wa mfano na ufanisi mkubwa.
“Dk. Samia anafanya kazi kwa kujituma na kuwajali wananchi, mimi binafsi nakuombea kura na ninaamini Watanzania wote tutaungana kumpa kura,” alisema.
Naye, Mgombea Ubunge wa Viti Maalumu anayewakilisha vijana, Lilian Mwacha, alisema vijana wa Arusha wana kila sababu ya kumuunga mkono Dk. Samia kutokana na matokeo makubwa katika utalii.
Amesema hali hiyo, imefanya ongezeko kubwa la watalii kutoka 600,000 hadi milioni tano hali iliyowezesha vijana wengi kunufaika na ajira.




