ATHNATH MKIRAMWENI NA
LILIAN JOEL, Arusha
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesisitiza umuhimu wa kulinda amani kama nguzo kuu ya ustawi wa taifa huku akitoa wito kwa wazazi na wananchi kuilinda kwa nguvu zote.
Pia, ametunuku kamisheni maofisa wanafunzi 296 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kwa cheo cha Luteni Usu na kushiriki mahafali ya sita ya shahada ya sayansi ya kijeshi, yaliyofanyika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi (TMA), Monduli mkoani Arusha.
Akizungumza baada ya kuwasili mkoani Arusha, Rais Dk. Samia, alisema mikoa ya Arusha na Manyara, imeendelea kuwa mfano wa utulivu kutokana na ushirikiano kati ya viongozi wa serikali, kimila, machifu na taasisi za dini.
Alisema hali hiyo, imewezesha shughuli za utalii na maendeleo mengine, kuendelea bila migogoro.
Rais Dk. Samia, alieleza kuwa misingi hiyo ya amani, ndiyo inayoifanya Tanzania iendelee kusonga mbele na kuwavutia wageni kutoka mataifa mbalimbali.
Akiwahutubia wananchi, Rais Samia, alisisitiza kuwa, amani ndiyo tumaini la Watanzania na uhai wa taifa, maisha, upendo, umoja na mshikamano, haviwezi kudumu bila kuwepo utulivu.
“Amani pekee ndiyo tumaini letu, uhai wetu ni amani yetu, maisha yetu ni amani yetu, ninawataka Watanzania kuithamini na kuilinda kama urithi muhimu,” alisema.
Pia, Rais Dk. Samia, aliwaomba wazazi wote nchini, kuzungumza na watoto na vijana, kuepusha mienendo inayoweza kuhatarisha amani, akibainisha kuwa, baadhi ya vijana, hujiingiza katika vitendo hatarishi kwa kushawishiwa bila kuelewa madhara yake.
“Haya mambo siyo ya kujaribiwa katika nchi na kuwataka wananchi kuendelea kuimarisha utulivu maeneo yao kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho,” alisema.
Akizungumza katika mahafali ya Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli, Rais Dk. Samia, alianza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuruhusu shughuli hiyo kufanyika kwa mafanikio.
Pia, alitoa pongezi kwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali John Jacob Mkunda, timu yake na viongozi wote wa chuo kwa kusimamia maandalizi na kuhakikisha mahafali hayo, yanafanyika katika mazingira bora na yenye heshima.
Vilevile, Rais Samia, alimpongeza Mnadhimu Mkuu wa Jeshi na Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi wa Chuo hicho, Luteni Jenerali Salum Othman, kwa uongozi thabiti katika kusimamia mafunzo ya kijeshi.
Alieleza kuwa, mafunzo hayo ni muhimu kwa jeshi na taifa kwa ujumla, kwani yanawaandaa wanajeshi kuwa na ubora na uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi mkubwa wa kulilinda na kulihudumia taifa.
Rais Samia, aliwapongeza wahitimu wa shahada ya sayansi ya kijeshi kwa juhudi, maarifa na nidhamu waliyoionesha wakati wa mafunzo yao.
WAZIRI WA ULINZI
Kwa upande wake, Waziri wa Ulinzi, Dk. Rhimo Nyansaho, alisema chuo cha Mafunzo ya Kijeshi, Monduli, kimepiga hatua kubwa kwa kuendelea kutoa wahitimu wa shahada ya kwanza ya sayansi ya kijeshi kwa kujisimamia.
Alisema mwaka huu wahitimu 106 wametunukiwa shahada na Rais Dk. Samia, huku akisema idadi ya wahitimu wanawake imeongezeka kutoka 21 hadi 25 mwaka huu.
Dk. Nyansaho, alisema ongezeko hilo, linaonesha jitihada za wizara katika kuimarisha uwiano wa kijinsia bila kuathiri ubora wa mafunzo.
Waziri huyo, alibainisha kuwa, uongozi makini wa Amiri Jeshi Mkuu, umeifanya JWTZ kuwa mfano wa ubora ndani na nje ya nchi, huku wahitimu wapya wakihakikishiwa kuwa wako tayari kulitumikia taifa kwa ujasiri, uadilifu na uzalendo.
Aliongeza kuwa, chuo kinaendelea kupanuka kimataifa baada ya kuanza kupokea wanafunzi kutoka mataifa rafiki, hatua inayothibitisha hadhi ya Tanzania katika utoaji wa mafunzo bora ya kijeshi.
Dk. Nyansaho, alisema mafanikio hayo ni matokeo ya maono ya Rais Samia na moyo wake wa kujitoa katika kuimarisha amani, usalama na maendeleo ya kijeshi na kijamii nchini.
Mkuu wa Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi (TMA), Monduli Meja Jenerali Jackoson Mwasoba, alisema jumla ya maofisa waliotunukiwa kamisheni ni 296 wakiwemo wanaume ni 257 na wanawake 39.
Aidha, alisema katika kundi la 06/22 la Shahada ya Sayansi ya Kijeshi BMS ni 106 na walipata mafunzo kwa muda wa miaka mitatu katika chuo cha TMA na 72/24 (Regular) ni 102, wamepata mafunzo kwa muda wa mwaka mmoja na maofisa wengine 89.
Alisema mwanafunzi aliyefanya vizuri katika fani zote kwa ujumla ni Taufiki Muhsin.
Hata hivyo, waliotunukiwa kamisheni maofisa wa jeshi ni 296 kwa cheo cha Luteni Usu na waliotunukiwa ni kundi la sita la mwaka 2022, waliohitimu shahada ya Sayansi ya kijeshi (BMS) na kundi la kawaida 72 la mwaka 2024 (Regular).
Maofisa hao, walitunukiwa kamisheni katika vyeo vipya vya Luteni Usu ni wanawake 39 na wanaume 257, ambao kwa pamoja, wanaunda jumla ya maofisa 296.
Katika idadi hiyo, maofisa 23 wanatoka mataifa ya Burundi, Comoro, Kenya, Malawi, Msumbiji, Rwanda, Uganda na Zambia na 89 ni maofisa wanafunzi Watanzania waliopata mafunzo kutoka nchi rafiki.




