Na ATHNATH MKIRAMWENI
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimewataka madiwani kufanya kazi zinazobeba ajenda za wananchi, zitakazotoa majawabu ya kero katika maeneo yao.
Pia, CCM imesema itaendelea kusimamia vyema misingi ya uadilifu kwa watendaji wa Chama.
Kauli hiyo ilitolewa na Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Kenani Kihongosi, jijini Dar es Salaam, alipozungumza na UHURU.
“Wito wangu kwa madiwani wote, mhakikishe mnatunga sheria ambazo ni rafiki kwa watu na sio kandamizi zitakazowaumiza wananchi, mkawe watetezi na washauri wa kulinda maslahi ya umma katika maeneo yenu,” alisema.
Kihongosi alisema Chama kitatoa miongozo ya namna bora ya kufanya kazi kwa madiwani wa CCM.
“Madiwani wakafanye kazi zinazobeba ajenda za wananchi ambazo zitatoa majawabu ya kero katika maeneo yao.
Kwa watakaokwenda kinyume na maagizo ya Chama, Chama kina utaratibu wake, kina vikao vyake katika ngazi husika iwapo mtu amekosea watamwita kwenye vikao na kufanya uamuzi ambao unakubalika kikatiba ndani ya Chama,” alisema Kihongosi.
Aliwataka madiwani hao kuwa mstari wa mbele kukisemea Chama kwa wananchi, kutokana na maendeleo yaliyopatikana nchini, chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Kwa upande wao, baadhi ya madiwani wa Mkoa wa Dar es Salaam, waliahidi kuwatumikia wananchi ipasavyo katika usimamizi wa miradi ya maendeleo.
Diwani wa Kata ya Kigogo (CCM), Manispaa ya Kinondoni, Nassib Limira, alisema amejipanga kutekeleza ahadi alizoahidi wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu mwaka huu.
“Tumeingia kazini rasmi, katika ahadi zipo za muda mfupi na mrefu, wananchi wa Kigogo wanipe muda niwatumikie.
Tuliahidi mambo mengi katika kampeni, mfano upanuzi wa shule ya sekondari na kituo cha afya, kwa hiyo hayo yote tunaanza kuyafanyia kazi mara moja,”alisema.
Diwani wa Kata ya Somangira (CCM), Manispaa ya Kigamboni, Juma Luja, alisema aliahidi ajira kwa vijana na miradi ya ujenzi wa barabara kazi ambayo imeanza.
“Sasa nakwenda kuwasimamia vijana wa kata yangu wenye sifa kuhakikisha wanaingia katika mchakato wa kupata ajira,”alisema.
Diwani wa Viti Maalumu (CCM), Manispaa ya Temeke, Nuru Cassian, alisema atasimamia mikopo ya asilimia 10 kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu iwafikie kwa muda sahihi.




