Na ELIZABETH JOHN
MAMLAKA ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), imeongeza zaidi ya vibali 70 vya muda kwa mabasi yanayosafiri kutoka Dar es Salaam kwenda mikoa mbalimbali nchini.
Imesema hatua hiyo imelenga kukabiliana na ongezeko la uhitaji wa usafiri kuelekea msimu wa sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya.
Akizungumza na UHURU, Ofisa Mfawidhi wa LATRA katika Kituo cha Mabasi cha Magufuli, Rukia Kibwana, alisema mwisho wa mwaka ni kipindi ambacho abiria huongezeka, hivyo mamlaka kuongeza idadi ya mabasi ni jambo la kawaida kuondoa msongamano.
“Hadi kufikia jana mchana, vibali zaidi ya 72 vilikuwa vimetolewa kwa mabasi ya ziada, hatua iliyolenga kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma bila usumbufu,” alisema.
“Hadi leo (jana) mchana tulitoa vibali zaidi ya mabasi 72. Usafiri mwingi ni jioni, unapoona watu wamejaa stendi wanakuja kusubiri mabasi yao na wengine wanawahi kukata tiketi,” alisema.
Rukia aliwataka wananchi kuwa na uvumilivu katika kipindi hiki cha mwisho wa mwaka, akieleza LATRA inafahamu idadi kubwa ya watu husafiri kwenda kuungana na familia zao mikoani, hivyo mamlaka inaendelea kusimamia na kuratibu uongezaji wa mabasi kadri inavyohitajika.
“Niwaombe sana wananchi kuwa na uvumilivu kwa sababu tunajua baadhi ya watu wanapenda kwenda kuwasalimia ndugu zao katika mikoa mbalimbali. Niwaombe kuendelea kutuamini,” aliongeza.
LATRA imekuwa ikitoa vibali vya muda kila kipindi cha msimu wa sikukuu na sherehe kubwa ili kuhakikisha upatikanaji wa usafiri unakuwa wa uhakika hususani mikoa ya kaskazini.




