Na ELIZABETH JOHN
MKUU wa Mkoa wa Njombe, Anthony Mtaka, amesisitiza umuhimu wa vijana na wananchi kuendelea kulinda amani kuwa ndiyo msingi wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Mtaka alisema hayo katika Ibada ya Kanisa la Waadventista Wasabato, Njombe Mjini alipokuwa akizungumza na waumini ambapo alieleza kwamba vijana wa kizazi kipya wana nafasi kubwa katika kulinda na kuimarisha misingi ya taifa.
“Vijana wetu wa Gen-Z wana wajibu wa kulinda amani ya Tanzania, hiki ndiyo kizazi kinachobeba matumaini na sura ya taifa letu,” alisema.
Mtaka alisisitiza hakuna taifa linaloweza kusonga mbele bila haki na uwajibikaji, huku akisisitiza amani ya Tanzania imekuwa matokeo ya jitihada za wananchi kutimiza wajibu wao kwa umoja.
“Amani ni tunda la haki na wajibu, ni msingi thabiti wa maendeleo yetu. Tunao wajibu wa kuilinda amani ya nchi yetu kwa wivu mkubwa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo,” aliongeza.
Katika eneo la usalama wa mkoa, Mtaka alisema Njombe inabaki kuwa miongoni mwa maeneo salama nchini na haina matishio ya uhalifu.
Alifafanua kuwa serikali ya mkoa inaendelea kuimarisha mifumo ya ulinzi wa watu na mali zao kuhakikisha wananchi wanaendelea na shughuli zao za uzalishaji bila hofu.
“Usalama wa mkoa wetu utatuongezea imani kwa wawekezaji kuendelea kuona Njombe kama sehemu sahihi ya kuweka mitaji yao,” alisema huku akiwataka wananchi kuungana kuzuia tafrani zinazoweza kuharibu mali au miradi ya maendeleo.
Aidha, Mtaka aliwasihi wananchi kujenga tabia ya kutoa taarifa mapema mara wanapotilia shaka hali inayoweza kuhatarisha amani katika maeneo yao, kwamba ulinzi shirikishi hauwezi kusimama bila ushiriki wa wananchi.




