Na AMINA KASHEBA
SERIKALI imetoa wito kwa wadau wa soka na Watanzania kuisapoti timu ya Taifa Stars, kuhakikisha inafanya vizuri katika fainali za Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2025), zitakazofanyikia nchini nchini Morocco.
Mashindano hayo yanatarajiwa kufanyika Desemba 21, mwaka huu hadi Januari 18, mwakani nchini humo ambapo Stars hivi sasa ipo Misri katika maandalizi ya mwisho.
Akizungumza Dar es Salaam, Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Neema Msitha alisema ni muda wa Watanzania kutumia fursa katika mashindano hayo kipindi Stars itakapokwenda nchini Morocco.
Alisema mbali ya kwenda kuwashangilia Stars, Watanzania wanapaswa kutumia vyema nafasi hiyo katika kupata fursa mbalimbali.
“Timu yetu ya Stars inaendelea vyema na maandalizi serikali chini ya BMT kwa kushirikiana na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).
“Wito kwa Watanzania ni muda mwafaka kuwaunga mkono Stars kwenda Morocco pale anapoona kuna fursa kwa sababu kuna mambo mengi nje ya kwenda kuishangalia timu yetu,” alisema.
Katibu huyo alisema kuna fursa mbalimbali za kiuchumi ambapo Watanzania wanapaswa kuzitumia vizuri kipindi wakirudi hapa nchini waziendeleze.




