Na MWANDISHI WETU
SERIKALI imesema ina matumaini makubwa, kikosi cha timu ya Taifa Stars kitafanya vizuri katika michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON 2025).
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, Gerson Msigwa, serikali na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), wamefanya maandalizi ya kutosha kuhakikisha timu inafanya vizuri zaidi msimu huu.
Msigwa alisema kuwa timu inaendelea na mazoezi nchini Misri ambapo kesho itatua Morocco tayari kwa michuano hiyo.
Alisema wamefanya maandalizi ya kutosha kuhakikisha timu hiyo inafanya vizuri zaidi msimu huu na kuweka rekodi ya aina yake.
“Tuna matumaini ya kuvunja rekodi na kuvuka hatua ya makundi kutokana na maandalizi tuliyoyafanya kwa kushirikiana na TFF.
“Timu ipo vizuri chini ya Kocha Miguel Gamond ambapo hivi sasa inafanya mazoezi ya mwisho kabla ya kutua Morocco tayari kwa mashindano na tumetoa kila kitu kuhakikisha wachezaji wanakuwa na morali ya kutosha,” alisema Msigwa.
Alisema wamewaalika wadau mbalimbali kwenda Morocco kuhakikisha wanakwenda kujifunza fursa mbalimbali watakazozitumia msimu ujao ambapo Tanzania itakuwa moja ya nchi mwenyeji.
Kwa upande wa Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Neema Msitha alisema Watanzania wanatakiwa kuwa mstari wa mbele kuipa sapoti timu hiyo iweze kufanya vyema katika michuano hiyo msimu huu.
Alisema mbali ya Watanzania kwenda kuishangalia Taifa Stars, lakini watapata kujifunza fursa mbalimbali ambazo watazitumia katika msimu ujao wa michuano hiyo.
Fainali hizo zinatarajiwa kufanyika kuanzia Desemba 21, mwaka huu hadi Januari 18, mwakani nchini Morocco.
Katika michuano hiyo, Taifa Stars imepangwa kundi C na timu za Nigeria, Tunisia na Uganda.
Taifa Stars inatarajia kutupa karata yake ya kwanza Desemba 23, mwaka huu dhidi ya Nigeria, Desemba 27 dhidi ya Uganda kabla ya kumalizikana na Desemba 30, mwaka huu.




