Na AMINA KASHEBA
BONDIA wa ngumi za kulipwa, Abdallah Pazi ‘Dullah Mbabe’ amewaita mashabiki na wadau wa mchezo huo kujitokeza kwa wingi katika pambano la ‘Boxing Fighting Championship’.
Dullah Mbabe atapanda ulingoni kuzichapa Daudi Mgaya katika pambano la utangulizi la raundi nane, uzito wa juu litakalofanyika Ukumbi wa Superdome uliopo Masaki, Dar es Salaam, Januari 30, mwaka huu .
Akizungumza Dar es Salaam, Dullah Mbabe’ alisema maandalizi yake yako vizuri na siku hiyo amejipanga kucheza mchezo mzuri hivyo wadau wajipange.
“Nawaomba wadau wa ngumi na mashabiki wajitokeze kwa wingi siku hiyo kwani nimewaandalia burudani nzuri ambayo watafurahi.
“Narudi katika ukubwa mwingine ambao kila mtu atashangaa kuniona maana nina kiu ya kucheza katika viwango vikubwa, hivyo mashabiki wangu wakae tayari kuniona, “alisema Dullah Mbabe’.
Bondia huyo alisema hivi sasa anaendelea na mazoezi ya kujiweka fiti huku akisubiri siku ya pambano ifike aoneshe kazi nzuri.
“Najua wadau wa ngumi wamenikosa kwa kipindi kirefu, nimejipanga sitowaangusha kabisa maana nina kiu ya kupata ushindi, “alisema Dullah Mbabe.




