LAGOS, NIGERIA
BONDIA wa ngumiu za kulipwa uzito wa juu duniani, Muingereza Anthony Joshua, amepata majeraha katika ajali ya gari iliyotokea jana katika barabara kuu ya Ogun jijini Lagos nchini Nigeria, ambapo watu wawili wamefariki dunia.
Kwa mujibu wa BBC, Polisi wa Jimbo la Ogun nchini humo, imesema kuwa Joshua, mwenye umri wa miaka 36 na mzaliwa wa familia yenye asili ya Sagamu nchini Nigeria, alipata majeraha madogo lakini yupo salama huku wengine waliokuwa wamejeruhiwa walikimbizwa hospitalini.
BBC imeeleza kuwa vyombo vya habari vya ndani (Nigeria), vimeripoti kuwa Joshua alikuwa nyuma ya dereva wakati gari lake aina ya Lexus, lilipogonga lori lililokuwa limeegeshwa.
“Mashuhuda walisema kuwa gari hilo lilikuwa na abiria wanne, akiwemo Joshua. Watu wake wa ulinzi walikuwa katika gari lingine lililokuwa nyuma yao kabla ya kutokea kwa ajali hiyo,” ilieleza BBC.
Polisi na vyombo vya habari vya ndani vinaendelea kufuatilia hali ya Joshua na pamoja na uchunguzi zaidi wa ajali hiyo.
Joshua alikwenda Nigeria baada ya kumaliza kuzichapa na Jake Paul katika pambano lisilo la ubingwa lililofanyika Desemba 19, mwaka huu nchini Uingereza.




