Na NASRA KITANA
RAIS Dk.Samia Suluhu Hassan, amempa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, maagizo matatu kuhusu Michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON), 2027, ambayo anapaswa kujifunza Morocco.
Miongoni mwa maagizo hayo ni kujifunza mbinu walizotumia Morocco katika mashindano ya AFCON mwaka huu, kuhakikisha Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ inatinga fainali ya mashindano hayo mwakani.
Mambo mengine aliyoagizwa Makonda, ni kupeleka barua yenye ujumbe kwa Rais wa Shirikisho la Soka Barani Afrika(CAF), Patrice Motsepe na kuhakikisha Tanzania inakuwa namba moja katika kukuza utalii kupitia michuano hiyo.
Makonda aliyataja mambo hayo katika Uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), alipokuwa akielekea nchini Morocco.
AFCON 2027 itafanyika katika nchi za Tanzania, Kenya na Uganda.
“Tumepata heshima ya kutumwa na Rais Dk. Samia kwenda nchini Morocco kupokea na kutimiza ndoto ya wapenzi wa mpira wa miguu siyo tu Afrika bali duniani, kijiti cha maandalizi ya AFCON 2027.
“Kwa utamaduni uliopo, nchi inayoandaa mashindano yanayofuata baada ya kuhitimisha mashindano yaliopo, hupewa nafasi ya kukabidhiwa na kuanza maandalizi ya michuano ya AFCON 2027.
Rais Dk.Samia amedhamiria kwa dhati na kwa nguvu zake zote kuiweka Tanzania katika ramani ya dunia katika michezo yote duniani,” alisema Makonda.
Waziri Makonda alisema Rais Dk. Samia amewaelekeza yeye, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Gerson Msigwa na ujumbe waliombatana nao kwenda nchini Morocco kufanya mambo hayo matatu.
“Jambo la kwanza, ametupatia barua mahususi ya kumpelekea Rais wa Shirikisho la Soka Barani Afrika(CAF), Patrice Motsepe yenye ujumbe mzito kutokana na kazi nzuri ambayo shirikisho hilo lilitambua kazi alioifanya Rais Dk. Samia ya kuwekeza katika michezo na kufikia hatua ya kumpa tuzo kama raisi bora aliyefanya kazi nzuri ya kuinua michezo ndani ya Tanzania kwa fedha nyingi za hamasa lakini, pia kwa kujenga miundombinu.
“Pili, Rais Dk. Samia ametutuma kwakuwa Morocco tulicheza nayo na Taifa Stars ikaleta ushindani wa hali ya juu, tukatazame na kujifunza mbinu zote walizonazo kuhakikisha Tanzania 2027, kama siyo kucheza fainali basi kombe linabaki nyumbani,”alisema Makonda.
Alisema kutokana na maelekezo hayo, waliambatana na wataalamu mbalimbali, ambao wengine tayari wapo nchini Morocco kujifunza mambo mbalimbali.
Aliongeza, wao wanakwenda kuendelea kuona mbinu walizotumia Morocco kuifanya timu yao kuendelea kushika hatamu na kutinga fainali ili Taifa Stars iendelee kuvunja rekodi kama ilivyokuwa kawaida yake.
“Jambo la tatu ambalo Rais Dk. Samia ametutuma; ni kwamba kwa kuwa Morocco hivi sasa ndiyo nchi inaongoza kwa utalii kupitia michezo kwa kushika namba moja hivyo, ametaka Tanzania ishike namba moja kwa kuwa ina fursa nyingi kuliko nchi yeyote Afrika hivyo kutakuwa na watu maalumu kwa ajili ya kuangalia hoteli, usafiri, vyakula, utalii kuhakikisha AFCON 2027 inaacha historia njema kwa watanzania kwa kuimarisha uchumi wao,” alisema Makonda.
Makonda alisema ni ndoto ya Rais Dk. Samia kwa kila Mtanzania aliyopo ndani na nje ya nchi, ambaye anayo fursa ya kusaidia na kusapoti mashindano hayo milango ipo wazi kwa wizara ya michezo.
MAANDALIZI
Alisema maandalizi ya AFCON 2027 yataanza tarehe 19, mwaka huu, baada ya kukabidhiwa kijiti Januari 18 katika fainali ya michuano hiyo kati ya Morocco na Senegal.
“Katika maandalizi haya tutakuwa na mashindano ya wasanii kutunga wimbo bora utakaotumika katika mashindano hayo, vikundi mbalimbali na ngoma zitakazoshindana kwa ajili ya mashindano haya,”alisema Makonda.
Katika AFCON 2025, Taifa Stars iliishia hatua ya 16 bora, baada ya kufungwa bao 1-0 dhidi ya mwenyeji Morocco.




