SELINA MATHEW, DODOMA
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Asha Rose Migiro, ametoa maagizo kwa wabunge na mawaziri, kuhudhuria vikao ngazi ya mashina kubaini changamoto zinazowakabili wananchi.
Dk. Migiro alisema hatua hiyo itawawezesha wabunge na mawaziri kuzipatia ufumbuzi changamoto mbalimbali zitakazoibuliwa katika vikao hivyo.
Katibu Mkuu alisema hayo jijini hapa, alipozungumza na mabalozi wa mashina Mkoa wa Dodoma.
“Itatuwezesha kubaini changamoto ambazo tuliahidi kuzifanyia kazi katika Ilani ya Uchaguzi baada ya kupokea dola. Mabalozi wa mashina ni chemichemi ya fikra, macho, masikio na daraja linalounganisha Chama na wananchi,” alisisitiza Dk. Migiro.
Alisisitiza: “Viongozi ngazi za juu, tufanye vikao vya kikatiba kupata changamoto za wananchi na tushauri Chama ili kiishauri Serikali.”
Alieleza lengo la mkutano huo ni kuimarisha imani ambayo Chama inayo kwa mabalozi kupitia mchango wao mbalimbali.
Dk. Migiro alisema Dodoma ni eneo lenye utulivu wa kisiasa, mshikamano wa wanachama na mwendelezo wa kazi za Chama.
“Uhai wa Chama ni safari ya kila siku ambayo inaanzia katika ngazi ya mashina, ndiyo sababu Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ametoa umuhimu wa kipekee kutuelekeza katika shughuli zetu tuhakikishe tunakuwa karibu na mabalozi
“Hakika mitaani Chama kinakutana ana kwa ana na maisha halisi ya wananchi. Katika mashina ndipo mahali penye uwazi, watu kukutana, kujadiliana, kuzungumzia masuala mbalimbali ya kijamii, uchumi na siasa bila kubagua itikadi yoyote,” alibainisha.
Pia, Dk. Migiro aliwasilisha salamu za shukrani kwa mabalozi kutoka kwa Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Dk. Samia kwamba anathamini na kutambua umuhimu wa mashina ndiyo maana alichukua hatua thabiti kuhakikisha wanapatiwa vitendeakazi.
Alisema katika kuimarisha sauti ya mabalozi, shina ni sehemu ya mkakati wa kupiga kura za maoni kuhakikisha sauti ya wananchi inasikika.
Katika hatua nyingine, Dk. Migiro alizindua Shina la Makunduchi lililopo Mtaa wa Uhuru Dodoma Mjini na kuwaomba wajumbe wa Shina hilo ambao ni wanaCCM na wasio CCM kuwa mfano katika jamii kupiga hatua ya maendeleo.
Dk. Migiro, aliwapongeza kukifanya ‘kijiwe’ hicho kuwa sehemu ya kujipatia kipato bila ya kujali itikadi zao.
Alisema hatua hiyo inaonesha umoja na kudhihirisha kuwa kuna shughuli lazima ziwalete wananchi pamoja.
“Shina hili niwapongeze, mmetuthibitishia kuwa shughuli za kiuchumi hazina itikadi, lakini katika kushirikiana hivi tunawavuta na kuwaleta pamoja Watanzania, wanajamii wenzetu bila ya kujali itikadi kwasababu maendeleo ya nchi hayana itikadi, umoja wa nchi hauna itikadi na umadhubuti wa taifa pia hauna itikadi
“Ni jukumu letu kuhakikisha tunashirikiana na jamii yote, maana kura tulizopigiwa zimepigwa na wanaCCM na wasio wana CCM, na Rais wetu ambaye ni Mwenyekiti wa Chama chetu ni Rais wa wote hivyo na sisi lazima tuwe ni watumishi wa wote,”alisema.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dodoma, Adam Kimbisa alisema Chama kipo tayari kukosolewa, kusahihishwa, lakini hakipo tayari kutukanwa au kubezwa.
Alisema hivi karibuni kumekuwa na matendo ya kubeza na kutukana jambo ambalo sio sawa na hawawezi kukubali.
“Chama hiki kina kiongozi wake imara na tunamuamini kuwa anatuongoza vizuri na ndio maana CCM ipo imara, tunakuomba kiongozi wetu lala usingizi Chama kipo imara, mabalozi wapo imara na mikoa ipo imara.
“CCM inapenda kukosolewa na hatuogopi kukosolewa wala kushauriwa kwa sababu wanaofanya hivyo wanatufundisha jambo na ndio maana tupo imara kwa sababu tunapokea ushauri lakini uwe usiobeza, “alisema.
Kimbisa alitoa wito kwa wanaobeza na kutukana kufanya shughuli za taasisi zao.
“Mi nitoe wito kwao wafanye shughuli za taasisi zao,sasa sijui taasisi zao hazitoshi, ni ndogo au wakisema ndani ya taasisi zao hawasikiki, sisi hatukubali tunataka kila mtu afanye kazi kwenye taasisi yake kama ya kidini, kijamii afanye kazi huko,”alisema.




