Na IRENE MWASOMOLA
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema serikali inatarajia kununua matrekta 10,000 na kuanzisha vituo jumuishi 1,000 vya huduma za zana za kilimo katika ngazi ya kata.
Dk. Mwigulu, alisema hatua hiyo, inalenga kuongeza tija, kupunguza gharama na kuwapa wakulima muda wa kushiriki shughuli nyingine za kiuchumi.
Waziri Mkuu, alitoa kauli hiyo, akifungua Mkutano wa Kwanza wa Kikanda wa Afrika wa Matumizi Endelevu ya Zana za Kilimo, unaofanyika jijini Dar es Salaam unaolenga kuweka msingi wa ushirikiano wa kikanda kuendeleza Ajenda ya Mfumo wa Zana Endelevu za Kilimo Barani Afrika (F-SAMA).
Dk. Mwigulu, alisema ni muhimu kuimarisha uwekezaji katika zana za kilimo rafiki kwa mazingira na zinazozingatia mabadiliko ya tabianchi.
“Zana hizi zinapaswa kupunguza uzito wa kazi, kuongeza tija, kupunguza upotevu wa mazao na wakati huo huo, kulinda mazingira kwa kutumia teknolojia zinazohimili athari za tabianchi kama ukame na mabadiliko ya misimu
“Tunapaswa kuhakikisha ushiriki mkubwa, wa makusudi wa sekta binafsi katika uzalishaji, usambazaji na utoaji huduma za zana za kilimo
“Serikali zetu zinapaswa kuweka mazingira wezeshi ya sera, sheria na vivutio vya uwekezaji ili sekta binafsi, ishiriki kikamilifu, kuongeza upatikanaji wa zana za kilimo na kupunguza gharama kwa wakulima,” alisema Waziri Mkuu.
Aidha, Mwigulu, alisema ni muhimu kuwawezesha vijana na wanawake kushiriki kikamilifu biashara, ubunifu na utoaji wa huduma zana za kilimo, kwa kuwa ni kundi lenye nguvu kazi, ubunifu na uwezo wa kuleta mabadiliko ya haraka, endapo litapatiwa mafunzo, mitaji, teknolojia na fursa za masoko.
Alisema uwezeshaji wa makundi hayo ni msingi wa maendeleo jumuishi na endelevu.
“Uwezeshaji huu, unapaswa kupimwa kwa viashiria mahsusi vya ajira, uanzishwaji biashara endelevu, ushiriki wa vijana na wanawake katika minyororo ya thamani ya zana za kilimo.”
Waziri Mkuu, alisema kupitia mkutano huo, nchi za Afrika kwa kushirikiana na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Umoja wa Afrika (AU), taasisi za fedha, sekta binafsi, watafiti na wadau wa maendeleo, zinakusudia kujenga mifumo thabiti ya huduma za zana za kilimo, inayokidhi mahitaji halisi ya wakulima wadogo na kati, kuimarisha uratibu wa taasisi na kubadilishana uzoefu.
Aidha, Dk. Mwigulu alitoa rai kwa nchi za Afrika, kuharakisha utekelezaji wa mifumo ya zana endelevu kwa kuunganisha kikamilifu na sera, mikakati na mipango ya kitaifa kwa kuwa itasaidia juhudi za pamoja kuchochea mabadiliko.
“Tuweke malengo yatakayopimika, ninaomba wadau wote, serikali, sekta binafsi, taasisi za tafiti kuchukulia masuala haya kama ajenda ya pamoja inayohitaji utekelezaji thabiti
Alisema Afrika imeanza kuchukua hatua madhubuti kupitia mifumo ya zana endelevu za kilimo, unaoandaliwa kwa ushirikiano wa Umoja wa Afrika na FAO kwa mtazamo jumuishi na endelevu.
Alipongeza FAO kuanza mchakato wa kuanzisha kituo cha umahiri wa zana za kilimo na serikali iko tayari kutoa eneo na ushirikiano kwa uanzishwaji wa kituo hicho nchini.
Dk. Mwigulu, alisema madhara yanayotokana na ukosefu wa zana za kilimo, huleta aibu kwa nchi za Afrika, akitoa mfano kipindi cha mzozo wa Russia na Ukraine, ambapo mataifa ya Afrika yalipata shida ya mafuta ya kupikia.
Dk. Mwigulu alifafanua, kutokana na neema ya ardhi na uwezo wa uzalishaji kwa nchi za Afrika, inatosha kuzalisha mazao ya aina yoyote na kulisha bara lake na dunia.
Aliongeza hali ya uwekezaji katika zana za kilimo barani Afrika haijaendana na mahitaji halisi ya wakulima wadogo na kati, kutokana na upungufu wa mitaji, mifumo dhaifu ya huduma, ukosefu wa ujuzi wa kiufundi na changamoto za upatikanaji wa matengenezo ya zana hizo.
Waziri Mkuu alisema athari za mabadiliko ya tabia nchi, ukiwemo ukame mafuriko na mabadiliko ya misimu ya mvua, zimeendelea kupunguza uzalishaji na kuongeza hatari ya ukosefu wa usalama wa chakula.
Dk. Mwigulu alisema pia ongezeko la ushindani wa matumizi ya ardhi kati ya kilimo, mifugo na masuala ya makazi ni miongoni mwa changamoto barani Afrika.
Alisema mkutano huo utakwenda kutafuta suluhisho la kuiondoa Afrika katika matatizo ya aina hiyo, kwa kuwa ni jukwaa la kimkakati linalolenga kuharakisha mageuzi ya mifumo ya uzalishaji chakula barani Afrika.
Pia, alisema kupitia mkutano huo nchi za Afrika kwa kushirikiana na FAO, taasisi za fedha, watafiti, sekta binafsi na wadau, zinakusudia kubadilishana uzoefu wa kisayansi na kujenga mifumo thabiti ya huduma za zana za kilimo zinazokidhi mahitaji.
“Mkutano huu pia unalenga kuweka msingi wa ushirikiano wa kikanda, katika kuendeleza ajenda ya mifumo ya zana endelevu za kilimo Afrika na mkakati wa mpango jumuishi wa maendeleo ya kilimo Afrika wa miaka 10 (2026/2035) wa kuzingatia masuala ya ujuzi, ajira kwa vijana,”alisema.
Dk. Nchemba alilipongeza FAO kwa mchango wao wa kukuza sekta ya kilimo, ambapo aliwashauri wawakilishi wa shirika hilo kutembelea vivutio vya Tanzania.
Naye Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, alisema, nii ni mara ya kwanza mkutano huo unafanyika nchini na barani Afrika.
Alishukuru FAO, taasisi nyingine na viongozi wa serikali kutoka mataifa mbalimbali kushiriki mkutano huo.
“Tumekusanyika hapa mataifa mbalimbali kutoka bara la Afrika kufanya mkutano wa kwanza kuhusu matumizi endelevu ya zana za kilimo,”alisema.
Chongolo, alisema kupitia mkutano huo, serikali imepanga kuzindua Mkakati wa Taifa wa Zana za Kilimo wa Awamu ya Pili (2026-2035).
Chongolo alisema mkakati huo umelenga kuimarisha matumizi, utengenezaji, uendelezaji, uhamasishaji, usimamizi na uratibu endelevu wa teknolojia zinazorahisisha kazi, kuokoa muda katika mnyororo wa uzalishaji na uongezaji wa thamani wa mazao ya kilimo.




