Na DUSTAN NDUNGURU, Songea
KATIBU wa NEC, Idara ya organaizesheni ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Issa Haji Gavu, amewataka wananchi wa Jimbo la Peramiho, mkoani Ruvuma, kujipanga kwa uchaguzi mdogo wa ubunge unaotarajiwa kufanyika Februari 26, mwaka huu, kwa kuendelea kukiunga mkono Chama kutokana na utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Gavu amesema hayo alipozindua kampeni za ubunge wa uchaguzi mdogo wa jimbo hilo zilizofanyika Kata ya Magagula, wilayani Songea Vijijini, mkoani Ruvuma.
Amesema kamwe wananchi wa jimbo hilo wasijaribishe kumchagua mbunge asiye sahihi, wakifanya hivyo watapoteza fursa muhimu, kwani mgombea anayetokana na CCM ndiye mtu sahihi kumchagua siku ya kupiga kura ikifika.
Katibu huyo aliwataka wananchi wa Peramiho wamchague Dk. Lazaro Komba, aendeleze kazi nzuri iliyofsnywa na mtangulizi wake Jenista Mhagama aliyefariki dunia Desemba 11, mwaka jana.
Kwa mujibu wa Gavu, wanachama wa CCM wanapaswa kuendelea kueneza mafanikio yaliyopatikana katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, maji, umeme, kilimo na mifugo, kumwezesha mgombea wa CCM kupita kwa urahisi katika uchaguzi huo.
Alisisitiza kuwa, CCM imejipanga kuendelea kuleta maendeleo katika sekta zote na imekuwa ikigusa maendeleo kwa Watanzania bila kubagua, hivyo kumchagua Dk. Komba ni kuchagua maendeleo.
“ CCM haitashinda katika uchaguzi huo kwa sababu ya mabavu bali itashinda kwa sababu ya umoja na mshikamano uliopo ndani ya Chama, sanjari na utekelezaji wa yale ambayo imekuwa ikiahidi wakati wa kampeni za uchaguzi,”alisema.
Alisema CCM inaamini wakati wote kuwa, suala la amani ni muhimu katika nchi na ndiyo maana Chama na serikali kimeendelea kusimamia, kikitambua bila ya amani hakuna shughuli za maendeleo ambazo zinafanyika katika nchi.
Kwa upande wake, mgombea ubunge wa jimbo hilo, Dk. Komba alisema hana shaka na ushindi wa Chama kutokana na kazi kubwa iliyofanywa na serikali ya CCM chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Dk. Komba alisema akichaguliwa kuongoza jimbo hilo atahakikisha anasimamia kwa vitendo utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi kwa kushirikiana na madiwani, watendaji na wananchi, maendeleo yanayokusudiwa yaonekane hilo ndilo lengo la Chama na serikali.
Aliwaomba wananchi wa jimbo kujitokeza kwa wingi Februari 26, mwaka huu, kukipigia kura Chama, ndicho Chama pekee nchini chenye nia ya dhati ya kuwaletea wananchi wake maendeleo ya kweli.




