Na MWANDISHI WETU
BODI ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPLB), imesema sababu ya kuupeleka mchezo wa ‘Dabi ya Kariakoo’ visiwani Zanzibar ni kutokana na Uwanja wa Benjamin Mkapa kuwa na matumizi mengine.
Yanga itakuwa wenyeji wa mchezo huo unaotarajiwa kufanyika Machi Mosi, mwaka huu katika Uwanja wa New Amaan, visiwani Zanzibar kuanzia saa 2:15, usiku.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa TPLB, Karim Boimanda alisema walipokea taarifa ya ombi la kuuhamisha mchezo huo kutoka Yanga na tayari walishawajibu.
Alisema wamekubali mchezo huo utafanyikia Uwanja wa New Amaan Complex, kwani unakidhi vigezo vya kanuni za soka, kutumika katika mechi mbalimbali zikiwemo za Ligi Kuu Tanzania Bara.
“Tuliandikiwa barua na Yanga kwenda kucheza mechi yao na Simba visiwani Zanzibar katika uwanja wa New Amaan Complex.
“Klabu inaruhusiwa kikanuni kuchagua uwanja mwingine kwenda kuchezea mechi zake kama uwanja wa awali unaweza kuwa na changamoto.
“Tumekubali mchezo ukafanyikie Zanzibar kwani uwanja unakidhi vigezo na Yanga wanaruhusiwa kikanuni kuhamisha mchezo kwenda sehemu nyingine.
“Tumejiridhishwa na uwanja kwani ule wa awali ambao ulitakiwa kutumika, utakuwa na shughuli nyingine,” alisema Boimanda.
Timu hizo, zilipambana Septemba16, mwaka jana ambapo Yanga iliichapa Simba 1-0 katika mchezo wa Ngao ya Jamii.
Bao la Yanga lilifungwa dakika ya 54 na Pacome Zouzoua aliwainua mashabiki katika viti baada ya kufunga bao la kuongoza kwa shuti kali akiwa ndani ya eneo la hatari.
Pacome alifunga bao hilo kufuatia kupokea mpira kutoka kwa Maxi Nzengeli.




