Na WILLIUM PAUL, Same
MAKAMU wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu, John Malecela, amesema suala la utalii mahali popote duniani linaendana na amani na utulivu.
Amewasihi wananchi kuhakikisha wanalinda amani kukuza utalii nchini na kuendelea kunufaika kupitia sekta hiyo.
Malecela alitoa kauli hiyo katika uzinduzi wa Tamasha la Same Utalii, lililofanyika kwenye viwanja vya Stendi wilayani Same, mkoani Kilimanjaro.
Alisema kuwa, baadhi ya nchi duniani zinaendeshwa kwa fedha za utalii, hivyo kuwataka wananchi kuitazama sekta hiyo kama fursa ya kukumbatia.
Kiongozi huyo alisema misingi ya utalii ni ukarimu kwa wageni na kuwataka wananchi wa Same kuwa mfano kwa ukarimu, kukuza utalii wilayani humo.
“Hata sehemu kukiwa na njiwa 10,000 wamejaa lakini jiwe likigonga tu wote wanakimbia, kwa hiyo na sisi utalii wetu uanze na sisi wenyewe Watanzania kuwa na amani, ni jambo la msingi. Amani ndio italeta na kuwakaribisha watalii na ndio itatufanya tuendelee kukua kiuchumi,” alisisitiza.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Utalii, Nkoba Mabula, alisema wizara hiyo inaunga mkono juhudi za Same kutangaza utalii na kwamba itaendelea kutoa ushirikiano kuendelea kuukuza.
Mkuu wa Wilaya ya Same, Kasilda Mgeni, alisema wilaya yake imejaliwa vivutio vingi vya asili na kihistoria vinavyoweza kuvutia watalii wa ndani na nje ya nchi na kwamba, lengo kuu la kuanzishwa kwa tamasha hilo ni kuhifadhi maliasili zilizopo.
Pia, kutangaza na kuendeleza vivutio vya utalii vilivyopo wilayani humo kuchochea maendeleo ya kiuchumi.
VIVUTIO
Alitaja baadhi ya vivutio hivyo ni Mlima Shengena, Kilele cha Mlima Kidenge, Maporomoko ya maji ya Thomthorn (Water Falls), Ziwa Ranzi na maeneo ya kihistoria kama majabali ya Mkumbavana na Makemane.




