NA MWANDISHI WETU
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Asha-Rose Migiro ameitaka Bodi ya Wadhamini ya Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere (MJNLS), kutekeleza mpango mkakati wa 2026/30 wa Shule hiyo ili kufikia malengo ya kuanzishwa kwake.
Kauli hiyo aliitoa alipofungua Kikao cha Bodi ya Wadhamini ya Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere (MJNLS) iliyopo Kibaha mkoani Pwani.
Dk. Migiro alisema katika mpango huo mkakati umeainisha vipaumbele vitano vikiwemo kuimarisha malezi ya kiitikadi na kiuongozi.
Alisema vipaumbele vingine vilivyopo katika mpango huo ni kuongeza uwasilishaji wa programu na umuhimu wa kuongeza matokeo ya utafiti na sera.
“Vipaumbele vingine katika mpango huo ni kukamilisha misingi ya taasisi, ikiwemo mifumo ya kidijitali na uhakiki wa ubora na kuhakikisha uendelevu kupitia ufadhili unaotabirika na matumizi yanayoakisi umiliki wa Vyama,”alisema.
Alisema vipaumbele hivyo vilivyopo katika mpango huo vinaipa Shule hiyo mwelekeo wa kutoka hatua ya mwanzo iliyofanikiwa hadi kuwa taasisi iliyokomaa, yenye dira na inayozalisha viongozi na mawazo kwa ajili ya uongozi.
“Hali hizi ndizo zinazoipa muktadha na umuhimu Mpango Mkakati wa 2026–2030 ulioko mbele yetu ambapo unatutaka kufikiri kuanzishwa kwa taasisi hii,” alisema.
“Kikao chetu cha Januari mwaka 2024 kilikuwa hatua muhimu ya mabadiliko wakati huo tulikutana kama Kamati Elekezi, tukiisindikiza taasisi iliyokuwa bado inaweka misingi yake na leo tunakutana ndani ya mfumo wa uongozi ulioimarishwa,” alisema.
Alisema kufuatia uzinduzi huo wa Bodi ya Uongozi na uanzishwaji wa mifumo muhimu ya kiutendaji hatua hiyo inawakumbusha funzo kuwa taasisi hukomaa kwa juhudi za makusudi.

“Kwa hiyo, kikao hiki kina wajibu wa vitendo zaidi ya kupokea taarifa, lazima tutoe mwelekeo na tufanye maamuzi yatakayogeuza Mpango Mkakati wa 2026–2030 kuwa programu hai ya utekelezaji — yenye ufadhili, matumizi na ufuatiliaji madhubuti,”alisema.
Alisema majadiliano hayo yanapaswa kutimiza mambo manne muhimu, ikiwemo kuthibitisha Shule kama taasisi ya kimkakati, kukubaliana juu ya ufadhili na matumizi yenye kuaminika.
“Kuimarisha nidhamu ya uongozi kupitia ratiba thabiti za vikao na mifumo ya ufuatiliaji na kutoa mwongozo wa kisiasa,” alisema.
Wajumbe waliohudhuria kikao hicho ni Katibu Mkuu wa Chama cha ANC (Afrika Kusini), Fikile Mbalula, Katibu Mkuu wa Chama cha FRELIMO (Msumbiji), Chaki Felizardo Passadas Aboobacar, Katibu Mkuu wa Chama cha ZANU-PF (Zimbabwe), Jacob Francis Nzwindamilimo Mudenda, Chama Cha SWAPO (Namibia), kimewakilishwa na Mjumbe wa Kamati Kuu, Dkt. Samuel Abraham Peyavali Mushelenga na Chama cha MPLA (Angola) kimewakilishwa na Mjumbe wa Kamati Kuu, Frederico Toth Jorge De Miranda.







