ATHNATH MKIRAMWENI NA IRENE MWASOMOLA
BAADHI ya wataalamu wa uchumi wametoa maoni tofauti, baada ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa matanki ya mafuta 15 ya kupokea mafuta katika Bandari ya Dar es Salaam.
Akizungumza na UHURU, Mhadhiri wa Uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Abel Kinyondo, alisema mradi huo utasaidia Tanzania kuwa na uchumi imara, hasa kunapotokea migogoro ya nje ya nchi inayosababisha bei ya bidhaa hiyo kupanda.
“Katika kipindi tulichopo hadi cha kati, uwekezaji huu ni muhimu sana kwasababu dunia hivi sasa ipo katika mitanziko mingi, moja kati ya namna ya ‘kudeal’ na mitanziko ni kuhakikisha una ‘storage’ kubwa,”alisema.
Amesema Tanzania ikiwa na sehemu kubwa zaidi ya kuhifadhi mafuta, nchi inaweza kwenda sokoni kununua mafuta na hivyo hata vita vya nje vikiibuka havitaathiri.
“Kama vita ya Ukraine inayoendelea Iran ikitokea, sisi tunakuwa ‘stable’ maana una ‘storage’ kwahiyo kuwa na hifadhi kunakupa ‘stability’,”alisema.
Aidha, Profesa Kinyondo, alishauri serikali kuendeleza jitihada za kuwekeza katika nishati mbadala, ikiwemo gesi kwa kuwa ndiyo suluhisho la kudumu hasa kipindi kunapotokea changamoto ya mafuta.
Kwa upande wake, Mhadhiri wa Uchumi wa Chuo Kikuu cha Zanzibar (SUZA), Profesa Haji Semboja, amesema Tanzania mradi huo utaimarisha uchumi na kudhibiti bei kipindi cha machafuko yanapotokea nchi za nje.
Profesa Semboja aliishauri serikali kuona namna ya kuendelea kuboresha sera na sheria katika usimamizi wa nishati hiyo kuongeza tija.
Mtaalamu wa uchumi, Fredy Naftari, alisema ujenzi wa matanki hayo utasaidia kuwa na hifadhi ya kutosha ya mafuta, hatua itakayoimarisha uchumi hasa katika kipindi cha misukosuko katika baadhi ya mataifa ya nje.
“Napongeza ujenzi wa matanki ni hatua nzuri kiuchumi, tukiwa na hifadhi kubwa ya mafuta, itasaidia nchi kuwa na akiba, kudhibiti uingizwaji holela wa mafuta na utakatishaji fedha,”alisema.
Naftari alisema ujenzi wa matanki hayo utasaidia shilingi ya Tanzania kuimarika, kwasababu mafuta yakiwepo nchini bidhaa hazitapanda bei.
Aidha, alimpongeza Rais Dk. Samia kuagiza kusomana mifumo ya Wizara ya Nishati, Wizara ya Uchukuzi, Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa kuwa itaboresha mazingira ya uwekezaji.
Mchambuzi wa uchumi, Dk. Yohana Lawi, alisema ujenzi wa matanki hayo utaongeza uwezo wa Bandari ya Dar es Salaam kuhudumia shehena za mafuta kwa ufanisi mkubwa.
“Mradi huo utasaidia kudhibiti mabadiliko ya bei za mafuta yanayosababishwa na misukosuko ya soko la dunia, kuwa na akiba kubwa ya mafuta kunatoa uhakika wa upatikanaji wake hata panapotokea changamoto za kimataifa,” alisema.
“Mradi huo unaotekelezwa bila mikopo ya nje unapunguza utegemezi, unaepusha mzigo wa riba na kuonesha kuwa taifa lina uwezo wa kugharamia miradi mikubwa kwa mapato yake,” aliongeza.
Alisema kuongezeka uwezo wa kuhifadhi mafuta kutapunguza muda wa kuhudumia meli na gharama za ucheleweshaji, hivyo kuongeza mapato ya bandari na serikali.
Alisema uwekezaji huo ni nguzo muhimu katika kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji wa nishati katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Mhadhiri wa Uchumi kutoka Chuo Kikuu Huria Tanzania (OUT) Dk. Timoth Lyanga, alisema ujenzi wa matanki hayo utasaidia kujenga uchumi imara unaojitegemea katika sekta ya nishati.
Dk. Lyanga alieleza miundombinu hiyo itaipa nchi uhakika wa nishati hata ikitokea migogoro au kupanda bei katika soko la dunia.
“Nchi yenye akiba ya kutosha haiyumbishwi kirahisi na mishtuko ya kimataifa, hatua hiyo itatoa muda wa kutosha kutafuta suluhisho endapo changamoto zitatokea,” alisema.
Akizungumzia maagizo ya Rais Dk. Samia ya kutaka mifumo isomane, Dk. Lyanga alisema itaimarisha uwazi, kuongeza ufanisi, kudhibiti mianya ya upotevu wa rasilimali na rushwa.
Kwa upande wake, Mchambuzi wa Masuala ya Uchumi na Uongozi wa Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Dk. Philip Daninga, alimpongeza Rais Dk. Samia kwa maono ya kujenga msingi imara wa maendeleo.
Dk. Daninga alisema mafanikio ya miradi mikubwa kama huo, inategemea uwajibikaji wa kila Mtanzania katika nafasi yake, taifa liendelee kusonga mbele kwa umoja, uzalendo na kujitegemea.
Juzi, Rais Dk. Samia aliweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa matanki 15 ya kupokea mafuta katika Bandari ya Dar es Salaam utakaogharimu sh. bilioni 678.6, ambazo zikijumlishwa na sh. bilioni 23.2 za thamani ya mkataba jumla ni sh. bilioni 701.8.




