Na MWANDISHI WETU
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameipongeza Hospitali ya Benjamin Mkapa iliyopo Dodoma kwa mageuzi na mafanikio makubwa katika utoaji huduma za matibabu ya kibingwa kwa wananchi.
Rais Dk. Mwinyi alisema hayo, alipokutana na Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo, Profesa Abel Makubi, Ikulu, Zanzibar.
Alisifu hatua kubwa ya utoaji huduma za kibingwa, yakiwemo matibabu ya figo, moyo na ubongo kufanyika nchini.
Rais Dk. Mwinyi alieleza hospitali hiyo umeipunguzia serikali na wananchi gharama za kuwapeleka wagonjwa kutibiwa nje.
Aidha, Rais Dk. Mwinyi alishauri uongozi wa hospitali hiyo, kuendeleza utaratibu wa matibabu ya nje kwa kuwafikia wananchi katika maeneo yao kupitia mpango wa ‘outreach programme’, kwa kuwa unasaidia kuwatibu wagonjwa wengi zaidi.
Pia, Rais Dk. Mwinyi aliahidi serikali kupitia Wizara ya Afya Zanzibar, itaendeleza ushirikiano na hospitali hiyo na kutafuta njia bora za kufanya kazi pamoja.
Pia, Rais Dk. Mwinyi aliipongeza hospitali hiyo kuendeleza mafunzo ya kuwajengea uwezo watendaji kupitia taasisi za ndani na wadau kutoka nje.
Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo, Profesa Makubi alisema wamepata mafanikio makubwa kipindi cha miaka 10 tangu kuanzishwa kwake, baada ya kutoa huduma za matibabu bobezi na kibingwa zaidi ya 20.
Profesa Makubi alitaja baadhi ni upandikizaji wa figo, upasuaji wa ubongo na matibabu ya moyo, hatua iliyochangiwa na jitihada za serikali kufanya mageuzi makubwa katika sekta ya afya.





